• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Wapwani wataka kummeza Yatani kuhusu Bandari

Wapwani wataka kummeza Yatani kuhusu Bandari

Na MOHAMED AHMED

AGIZO la kuanzisha upya shughuli ya kumtafuta mkurugenzi mkuu wa bandari ya Mombasa limezua mjadala mkali miongoni mwa wakazi wa Pwani.

Baadhi ya viongozi wa kisiasa na mashirika ya haki za binadamu wameeleza kughadhabishwa kwao na hatua ya waziri wa Fedha, Bw Ukur Yatani kuikataa orodha ya wanaotaka nafasi hiyo akisema kuwa hakuna aliye na uwezo huo.

Katika matokeo hayo watu watatu akiwemo aliyekuwa mkurugenzi mkuu wa mradi wa Lappset Silvester Kasuku, aliyekuwa katibu mkuu wa Ugatuzi Mwanamaka Mabruki na aliyekuwa kamishna wa tume ya polisi Murshid Mohammed, walikuwa wamefikia hatamu ya mwisho ya kazi hiyo.

Kadhalika, Bw Yatani, mnamo Jumanne alisema watatu hao hawakufikisha asilimia 70 ya alama, ambayo mtu anayetaka nafasi hiyo anapaswa kuipata.Mwenyekiti wa kitaifa wa kundi la Taireni Association of Mijikenda, Bw Peter Ponda alidai kuwa hatua hiyo ilichukuliwa kwa sababu Wapwani wawili walikuwa kwenye orodha ya watatu hao.Bw Mohammed na Bi Mwanamaka ni wakazi wa Pwani.

Bw Ponda alidai kuwa hatua hiyo ni mpango wa kuzima Wapwani kuchukua nafasi hiyo.“Haya yote yanafanyika kwa sababu ya maslahi ya wale walioko kwenye uongozi wa serikali kuu. Wanataka kuweka mtu wao na kwa sababu kwenye orodha ya hivi majuzi mtu wao hayuko ndiyo maana wanaanza upya,” akasema Bw Ponda.

Aliongeza: “Kitendo hiki ni jambo la kusikitisha. Hii bandari iko Pwani hivyo basi mtu wa Pwani anapaswa kupewa nafasi hii.”

Mkurugenzi wa shirika la Haki Afrika, Hussein Khalid alishangaa iweje shughuli hiyo irejelewe bila sababu mwafaka kuwekwa wazi.Alisema kuwa kuna haja ya wakuu serikalini kutoingilia kati suala hili la kuchaguliwa kwa mkurugenzi wa bandari.

“Kila sehemu nchini humu wakazi wa eneo fulani wanapaswa kupewa kipaumbele. Sisi kama shirika tumeona jambo hili limefanywa kimakusudi kwa sababu kuna Wapwani wawili ambao walikuwa kwenye orodha hiyo,” akasema Bw Khalid.

Bw Yatani alikuwa amedai kuwa watatu hao hawakupata alama hiyo na kuagiza shughuli nzima ifanywe upya.Jana, halmashauri ya bandari (KPA) iliweka tangazo kwenye magazeti na kutangaza kuwa shughuli hiyo itaanza upya na kuwataka wale wanaotaka nafasi hiyo kufikisha stakabadhi zao kabla ya Machi 19.Hii itakuwa mara ya tatu kwa shughuli hiyo kurejelewa.

Mwaka jana, Bw Yatani pia aliagiza shughuli hiyo irejelewe akisema kuwa kuna upendeleoa Siasa za hapo bandarini pia zilikuwa zimetawala shughuli hiyo.

Akizungumza wakati wa ziara ya kinara wa ODM Raila Odinga Pwani, Seneta wa Mombasa Mohammed Faki alisema kuwa bandari ndiyo sura ya watu wa Pwani na kuna haja ya Mpwani kuchukua nafasi hiyo.

“Hivi sasa hakuna mkurugenzi mkuu na juzi tumesikia kuwa kuna mambo ambayo hayakuwa sawa lakini sisi tunaomba kuwa mtu wa Pwani ndiye anayefaa kushikilia nafasi ile.”

Alimuomba Bw Odinga kusukuma mazungumzo hayo kwa Rais Uhuru Kenyatta kuhakikisha kuwa Mpwani anachukua usukani huo.

You can share this post!

Mpango wa kusafisha Pwani wazinduliwa

Raila asihi Wapwani wapitishe BBI