• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Mitihani ya kitaifa ya Gredi 4 yaanza Jumatatu

Mitihani ya kitaifa ya Gredi 4 yaanza Jumatatu

FAITH NYAMAI na DERICK LUVEGA

MITIHANI ya kutathmini wanafunzi wa Gredi ya Nne inaanza Jumatatu Machi 8. Mitihani hiyo itakuwa sehemu ya matokeo yatakayotumiwa kuamua iwapo watajiunga na shule ya upili baada ya gredi ya sita au la.

Waziri wa Elimu, Prof George Magoha amewataka walimu kuchukulia shughuli hiyo kwa umuhimu mkubwa kwa kuwa itakuwa na asilimia 20 ya alama za mitihani itakayozingatiwa katika gredi ya sita.

Mitihani hiyo imebuniwa na Baraza la Taifa la Mitihani Kenya (Knec) na wanafunzi watatathminiwa na walimu wao na matokeo kuwekwa kwenye tovuti ya Knec.

Shule zinatakiwa kumaliza mitihani hiyo na kuweka matokeo katika tovuti hiyo kati ya Machi 8 na Machi 19.

Prof Magoha alisema kwamba Knec itatoa vifaa vinavyohitajika kwa shule zote kufanikisha shughuli hiyo.

“Tayari KNEC imetoa mwongozo kuhusu mitihani hii muhimu ambayo ni sehemu ya utekelezaji wa mtaala mpya wa Competency Based Curriculum (CBC),” alisema.

Afisa Mkuu Mtendaji wa KNEC, Mercy Karogo alisema maandalizi ya mitihani hiyo yamekamilika.

“Vifaa vya kufanya tathmini hiyo viko tayari kwa kuwa shule zitavipata katika tovuti na kutekeleza shughuli hiyo kwa kufuata mwongozo uliotolewa,” alisema Dkt Karogo.

Mitihani ya gredi ya nne, tano na sita inatarajiwa kujumuisha asilimia 60 ya matokeo ya kitaifa ya wanafunzi hao watakapohitimu gredi ya sita.

Mtihani wa gredi ya nne utakuwa wa kwanza chini ya CBC jinsi lilivyoshauri Jopokazi kuhusu utekelezaji wa mtaala huo mpya wa elimu.

“Shule zinahitajika kuwasilisha matokeo ya mitihani ya wanafunzi ambao kwa sasa wako gredi ya nne kwa KNEC ambayo itakuwa asilimia 20 ya tathmini ya mwisho katika gredi ya sita,” unaeleza mwongozo huo.

Miongoni mwa masomo ambayo yatashirikishwa ni Hisbati, Kiingereza, Kiswahili, Lugha ya Ishara, Sayansi na Teknolojia, Kilimo, Muziki na Sanaa, Somo la Jamii, Somo la Kidini na Afya.

Afisa Mkuu Mtendaji wa Tume ya Walimu (TSC), Bi Nancy Macharia aliwataka maafisa wote wa elimu kusaidia shule kuhakikisha walimu hawatatiziki kupata vifaa vya kutumia kutoka kwenye tovuti ya Knec.

“Ninataka kusisitiza kuwa mitihani hii itafanywa wakati wa kawaida wa masomo na wanafunzi hawafai kuwekwa katika mazingira tofauti na waliyozoea katika darasa kila siku,” alisema.

You can share this post!

ODM: Raila anachezwa

Uhuru aamuru ardhi ya KDF irejeshewe jamii ya Samburu