• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 11:28 AM
FAUSTINE NGILA: Tujizoeshe maisha ya dijitali

FAUSTINE NGILA: Tujizoeshe maisha ya dijitali

Na FAUSTINE NGILA

NAWASHANGAA baadhi ya walimwengu kulia kuwa wamechoka kufanyia kazi nyumbani, wamechoka kutumia teknolojia; eti sasa wanaomba waruhusiwe kurudi kufanyia kazi ofisini.

Mataifa mengi bara Ulaya yalifungwa kuzuia maambukizi ya virusi hatari vya corona, na hivyo kuwafungia watu wajumbani mwao.

Inatamausha kwamba watu hao wanatamani kurudi kufanya kazi katika mazingira ya ofisi. Ni mwenendo ambao pia mimi nimeuona hapa Kenya.

Pindi tu baada ya serikali kulegeza masharti ya kuzuia maambukizi ya virusi hivyo, vinavyosababisha ugonjwa wa Covid-19, watu walirudi kujaa tena ofisini kama zamani.

Hii ni ithibati kuwa licha ya janga hili kufumbua ulimwengu macho kutambua kuwa ajira za usoni zitategemea teknolojia, Wakenya bado wamekwama katika fikra zilizopitwa na wakati.

Huwezi kuniambia miaka mitano ijayo bado utakuwa ukifanyia kazi ofisini, utakuwa ukisafiri hadi jijini kwa ajili ya ajira. Kufanya hivyo ni kuonyesha kuwa hakuna ulifunzalo kwa kila aina ya mapinduzi.

Ni mwaka mzima tangu corona itokee na kisha kutua hapa nchini. Unapaswa kuwa umejipanga kuunda ofisi yako nyumbani, ukazoea kuwahudumia wateja mitandaoni, kulipwa kwa majukwaa ya kidijitali na kupiga sala mitandaoni.

Iweje hadi sasa bado unaamini ajira itasalia ilivyo? Nakerwa na maelfu ya kampuni ambazo zimezembea kuwaelimisha wafanyakazi wake kuhusu mustakabali wa ajira dijitali.

Kampuni hizi hazijaweka mikakati ifaayo kuwezesha wafanyakazi kuendesha biashara nyumbani. Hawana vipakatalishi, hawana intaneti, wala kampuni hazijanunua programu za kisasa za kuratibu na kufuatilia utendakazi.

Kampuni zipo tu! Zinategemea mifumo ya zamani kama vile kufuatilia wafanyakazi kama wamefika kazini.

Hazina habari kuwa kwa kutumia programu hizo za kisasa unaweza kufuatilia kila mfanyakazi kwa urahisi zaidi na kujua anafanya kazi kiasi gani, amefikia malengo au la.

Watu wengi nikiwauliza masuala haya wanasema kuwa wamechoka kuona marafiki zao kwenye video za mawasiliano, wangetaka wakutane nao uso kwa macho.

Hilo linakubaliwa; lakini haifai kuwa ndio mtindo, iwe mara moja tu kwa miezi kadhaa. Dunia ya sasa inakwenda kwa kasi mno, yule anayetaka kufanya mambo kama mwaka uliopita atapitwa. Ni wakati wa kubadilisha fikra kabisa.

Usidhani kuwa baada ya watu kuchanjwa eti sasa teknolojia itarudi nyuma hadi hali ilivyokuwa kabla ya janga la corona. Ukweli ni kuwa utajionea teknolojia za uwezo mkuu hata zaidi kufikia mwisho wa mwaka huu.

Fikiria hivi. Je, iwapo janga lingine lingetokea duniani na kulazimisha kila mtu kufungiwa mahali bila kutangamana hata na familia, utaweza kuvumilia na kuponea kifo?

Ni wakati wa kufanya mambo ni kana kwamba kuna janga lingine njiani. Jifunze kutumia teknolojia zote kufanikisha maisha yako bila usaidizi wa mtu yeyote. Jiandae kwa maisha ya teknolojia tupu katika kila ulifanyalo.

Tumia mtandao kufanya utafiti ujue ni kifaa kipi kitakufaa zaidi kwa kazi yako, huduma gani itakupunguzia gharama. Haya yote yamejaa kwenye intaneti; anza kuitumia sasa.

You can share this post!

CHARLES WASONGA: Wakuzaji kahawa wapate hamasisho kuhusu...

WANDERI KAMAU: Tutajinasua vipi kutoka kwa usahaulifu wetu?