• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 11:14 AM
Duka la Nakumatt linavyohudumia wateja kisiri Nairobi

Duka la Nakumatt linavyohudumia wateja kisiri Nairobi

NA BRIAN WASUNA

Wakati msimamizi wa Nakumatt, Peter Opondo Kahi aliyauza matawi sita yaliyosalia kwa Naivas kwa Sh422 milioni, wengi walidhani kuwa Nakumatt imeisha kabisa. Aisee walikuwa wamekosa. Tawi moja la Nakumatt limekuwa likiendesha shughuli zake kisiri juu ya tawi la Naivas Prestige Plaza, Barabara ya Ngong, Nairobi huku likiuza bidhaa kwa bei nafuu ajabu.

Prestige Plaza ni mojawapo ya maduka sita ambayo Naivas ilichukua kutoka Nakumatt. Cha kushangaza ni kwamba, wathamini waliweka bei ya maduka hayo sita, fanicha kuwa Sh110.5 millioni huku Naivas ikigharamia mara nne zaidi ya fedha ambazo zilifaa.

Uzabuni wa Chandarana, muuzaji mwingine pekee aliyekuwa akimezea matawi haya sita mate, ulikuwa wenye dhamana ya Sh246 milioni.

Matawi haya sita yalikuwa Prestige Plaza, Lavington Curve, Highridge na Mega- yote yakiwa kwenye mji wa Nairobi na maduka makuu ya Nakumatt yaliyo kwenye miji ya Nakuru na Kisumu.

Jambo ambalo lisilojulikana na wengi ni kuwa Nakumatt ilisalia na duka moja ndogo ambalo lipo kwenye ghorofa ya kwanza juu ya Naivas ya Prestige Plaza.

Duka linalofanya kazi

Katika vitabu vya uratibu vya Nakumatt vilivyowasilishwa kortini na Bw Kahi, duka hilo halipo kwenye orodha ya mali ya Nakumatt ambayo yanaendelea kuendesha shughuli zake. Bw Kahi ameomba korti kuongeza mwaka wake wa uongozi kama msimamizi wa Nakumatt ili kumwezesha kufuatilia kesi za korti ambazo zitawezesha Nakumatt kujipatia milioni kadhaa ambayo itasaidia kupunguza deni.

Kwanza wakati ambapo Taifa Leo Dijitali ilimuuliza Bw Kahi kuhusu duka lililo kwenye ghorofa ya Prestige,  alisema kuwa nafasi pekee ambayo Nakumatt ilikalia kwenye ghorofa hiyo iliuziwa maduka ya Naivas.

Hata hivyo, Kahi alisema kuwa Nakumatt imekuwa ikikodi nafasi katika stoo ya Prestige Plaza ili kufanya kazi za kiofisi pekee baadaye. Hii ni baada ya Nakumatt kufukuzwa kutoka makao yao makuu katika Barabara ya Mombasa.

Makao hayo makuu yaliuzwa ili kufidia mikopo. Taifa Leo Dijitali ilimfahamisha Bw Kahi kuhusu stoo ya Nakumatt inayofanya kazi lakini akasema kuwa stoo hiyo iliyoko kwenye ghorofa ya Prestige huuza bidhaa kuu kuu ambazo zimetoka kutoka matawi ambayo yaliyondolewa.

Hata hizyo, mwandishi huyu aligundua kuwa maski ambazo zilitengenezwa mwezi uliopita zilikuwa baadhi ya bidhaa kwenye stoo hiyo, ishara kuwa lazima maski hizo zilikuwa zimenunuliwa kabla hazijawekwa mle kabatini.

Sanduku la maski

Bw Kahi alikataa kutia saini cheki za uidhinishaji wa akiba mpya, baada ya Taifa Leo Dijitali kumfahamisha kuhusu ununuzi wetu ambao ulikuwa pamoja na sanudku la maski ambazo zilitengenezwa mnamo Februari 9.

Msimamizi huyo alisema kuwa angechunguza jambo hilo. Baadhi ya bidhaa ambazo zinauzwa katika stoo hiyo zinaupunguzo wa hadi asilimia 90.

Risiti iliyopatikana kutoka mmoja wa wanunuzi inaonyesha kuwa shughuli zote ziko chini ya utawala. Hii inamaanisha kuwa shughuli zote zinasimamiwa na bw Kahi, ambaye alipewa jukumu la kufilisi biashara za Nakumatt na kuzifidia deni za wale waliowakopea.

Karatasi za korti zinaonyesha kuwa bw Kahi ameweza kufidia deni za Nakumatt zenye kiasi cha bilioni 5.1. Hii ina maana kuwa Nakumatt bado inawadai wauzaji na mashirika mengine bilioni 12.9.

“Hatuuzi. Tulienda huko sababu ofisi yetu kuu ilinadiwa na benki. Ni nafasi tu ya ofisi. Hakuna bidhaa mpya. Bidhaa zote ambazo zinauzwa zinatoka matawi yale makuu kuu,’ bw Kahi akaeleza timu ya Taifa Leo Dijitali.

Bidhaa zilizopunguzwa bei sana

Tunapotembea ndani ya stoo, wanaume wawili wanabeba makochi ya ngozi.

“Hii inatoka sh.85,000. Ipo kwenye punguzo la bei na ngozi yake ni nzuri sana. Bidhaa zinanunuliwa kwa haraka sana hivi basi ni bora uharakishe iwapo umependezwa,” mmoja wa wauzaji akasema tulipokuwa tunazunguka ndani ya stoo.

Idhibati ya namna duka la Nakumatt lilianguka tena kwa mpigo, ni ukiangalia baadhi ya bidhaa zilizopunguzwa bei. Makabati ya mbao ambayo mwanzo yaliuzwa kabati moja kwa sh. 24,000, sasa yanauzwa nusu ya bei hiyo. Bidhaa za kusafisha madirisha ambazo zilikuwa zinatoka sh. 1,195 sasa zinauzwa sh.800.

Katika sehemu ya vifaa vya watoto vya kuchezea, maski za mwanafilamu wa Marvel ambazo zilikuwa zawafanya watoto wengi kuzimezea mate zilikuwa zinauzwa kwa bei ya sh. 3,850 kabla Nakumatt kuanguka. Sasa zinauzwa sh. 600.

Bidhaa zingine ambazo zinauzwa kwa bei iliyopunguzwa ni kompyuta, sweta, fanicha, vitu vya jikoni, vifaa vya kamera vya usalama na vifaa vya kucheza muziki.

Bidhaa zinazonunuliwa kwa haraka hazipo

Stoo hiyo haiuzi bidhaa zinazonunuliwa kwa haraka kama mkate, maziwa na mafuta ya kupika. Baadhi ya bidhaa ambazo zilikuwa zinaletwa kwenye stoo hiyo wakati ambapo Taifa Leo Dijitali ilikuwa imezuru, zilionyesha kuwa kuna uwezekano wa bidhaa zingine nyingi zilizohifadhiwa kwenye maghala ambayo yalimilikiwa na Nakumatt hapo awali. Hali kadhalika, bidhaa hizi zinaweza wekwa kwenye makabati.

Kuwepo kwa vifaa vya kujilinda kama vile maski na vikingo vya uso ambazo zipo kwenye ofa katika stoo hiyo ni ishara kuwa yule ambaye anaendesha stoo hiyo amewekeza bidhaa hizo hivi majuzi.

Zaidi ya miezi miwili kabla Kenya kurekodi maambukizi yake ya kwanza ya ugonjwa wa Covid-19, Nakumatt iliondoka kwenye biashara ya uuzaji biadhaa mnamo Januari mwaka jana.

Vikingo vya kawaida vya uso, maski za KN95 na baadhi ya vifaa vya kujilinda vinapatikana kwa bei nafuu katika stoo hiyo.

Tulinunua sanduku moja ya maski za Naxsafe ambazo zilitengenezwa mnamo Februari 9, 2021 na ambazo zilikuwa zinauzwa kwa sh.295. Keshia alitupatia risiti ya Nakumatt.

Hata ingawa hati za risiti hizo zinafanana na zile za kitambo za Nakumatt, yaonyesha kuwa stoo hiyo inaweza kuwa chini ya kampuni inayomilikiwa na bw Shah.

Risiti hiyo ilitolewa na Parkview Shopping Arcade Ltd mojawapo ya kampuni ambazo benki ya UBA inafuata kuhusiana na deni ya milioni 119.

TAFSIRI: WANGU KANURI 

You can share this post!

Kituyi arejea nyumbani kusaka baraka za urais

Dkt Immanuel Gitamo: Mwanajeshi kutoka Kitale anayepiga...