• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 1:13 PM
Zaidi ya watu 3000 wakumbwa na uhaba wa maji Lamu Mashariki

Zaidi ya watu 3000 wakumbwa na uhaba wa maji Lamu Mashariki

Na KALUME KAZUNGU

ZAIDI ya wakazi 3000 wa vijiji vya Siyu, Shanga-Ishakani na Shanga-Rubu kwenye kisiwa cha Pate, Kaunti ya Lamu wanakumbwa na uhaba wa maji.

Wakazi wa vijiji hivyo tangu jadi wamekuwa wakitegemea maji ya mvua yanayohifadhiwa kwenye matangi maalum yanayotambulika na wenyeji kama jabia.

Wakazi pia hutegemea maji kutoka kwa visima.

Aidha tangu kiangazi kilipoanza kushuhudiwa kwenye maeneo mbalimbali ya Lamu, idadi kubwa ya majabia na visima vimekauka, hivyo kuwaacha wakazi bila maji.

Ni visima vichache ambavyo kwa sasa vimesalia kutoa maji ilhali vingine maji yake yakibadilika kuwa ya chumvi.

Katika mahojiano na wanahabari kwenye vijiji husika, wakazi walisema mara nyingi wamelazimika kuamka alfajiri kuelekea kisimani ili kuchota maji na kuepuka milolongo mirefu.

Wengine wamekuwa wakitembelea visima usiku wa manane ilmradi wachote maji bila kero la milolongo mirefu.

Kwenye kijiji cha Siyu ambacho kina karibu watu 2000, ni kisima kimoja pekee kinachotoa maji safi.

Bi Aisha Kassim aliiomba serikali ya kaunti na wahisani kuwasambazia maji kupitia malori ili wapumzike mahangaiko wanayopitia wakitafuta rasilimali hiyo.

“Wengi wetu hatulali usiku hapa. Tunakesha kisimani kusubiria maji. Kisima ni kimoja tu kinachotoa maji safi hapa Siyu. Visima vigine vimekauka ilhali baadhi vikitoa maji ya chumvi. Serikali ituonee imani,” akasema Bi Kassim.

Abdalla Yusuf alisema mara kwa mara wamekuwa wakilazimika kukodisha pikipiki ili kwenda kuchota maji eneo la Faza ambalo liko zaidi ya kilomita 30 kutoka Siyu.

Bw Yusuf anasema mtungi wa lita 20 wa maji huuzwa kwa hadi Sh50, bei ambayo wengi hawawezi kuimudu.

“Ukikosa nafasi ya kuchota maji kisimani basi hutakuwa na budi ila kuagiza maji kutoka Faza. Unakodisha pikipiki. Isitoshe, maji yenyewe unayanunua kwa bei ghali ya hadi Sh 50 kwa kila mtungu wa lita 20. Tunateseka,” akasema Bw Yusuf.

Katika vijiji vya Shanga-Rubu na Shanga-Ishakani, wakazi wamelazimika kutumia maji ya chumvi kutoka visimani.

Bi Mwanaisha Bamkuu alieleza hofu kwamba huenda wakaugua maradhi ya tumbo kutokana na matumizi ya maji chafu.

“Ukiangalia watoto na watu wazima hapa meno yao yameharibiwa na haya maji ya chumvi. Meno yako na rangi ambayo haiondoki. Watoto wetu pia wako na maradhi ya ngozi kutokana na matumizi ya haya maji chafu,” akasema Bi Bamkuu.

Vijiji vingine ambavyo uhaba wa maji unaendelea kusheheni ni vile vya msitu wa Boni, ikiwemo Milimani, Mangai, Mararani, Basuba, Bodhai na Kiangwe.

Kwa upande wake, Meneja wa Bodi ya Kusambaza Maji, Kaunti ya Lamu (LAWASCO), Kimani Wanaina alisema uhaba wa maji unaokumba baadhi ya vijiji vya eneo hilo umesababishwa na kiangazi kinachoendelea.

“Kiangazi kimepelekea baadhi ya mabwawa yetu kukauka, hivyo kupunguza kiwango cha maji kinachosambazwa Lamu kila siku. Natumai hali itarejea kuwa ya kawaida punde kiangazi kitakapofikia kikomo,” akasema Bw Wainaina.

You can share this post!

BIASHARA MASHINANI: Kijana anayechuma hela kwa uchapishaji...

BIASHARA MASHINANI: Mwalimu aliyeona nafasi ya ujasiriamali...