• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
Newcastle United na Aston Villa waridhika na sare katika gozi la EPL

Newcastle United na Aston Villa waridhika na sare katika gozi la EPL

Na MASHIRIKA

BAO la dakika ya mwisho wa kipindi cha pili kutoka kwa Jamaal Lascelles lilisaidia Newcastle kuwalazimishia Aston Villa sare ya 1-1 katika mechi ya Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) iliyochezewa uwanjani St James’ Park mnamo Ijumaa usiku.

Matokeo hayo yaliwezesha Newcastle kuweka hai matumaini finyu ya kuepuka shoka la kuwateremsha ngazi kwenye kampeni za EPL msimu huu.

Chini ya kocha Steve Bruce, Newcastle kwa sasa wanashikilia nafasi ya 16 kwa alama 28, mbili zaidi kuliko Brighton ambao kwa pamoja na Fulham, West Bromwich Albion na Sheffield United, wako katika hatari ya kushushwa daraja mwishoni mwa kampeni za msimu huu.

Villa waliwekwa kifua mbele na mwanasoka Ciaran Clark aliyejifunga kwa upande wa Newcastle baada ya kuzidiwa ujanja na Ollie Watkins katika dakika ya 86. Hata hivyo, Lascelles aliwasawazishia Newcastle sekunde chake kabla ya kipenga cha kuashiria mwisho wa mchezo kupulizwa.

Goli lililopachikwa wavuni na Lascelles lilichangiwa na kiungo Jacob Murphy aliyeshuhudia makombora yake mawili yakigonga mwamba wa lango la wenyeji wao.

Alama moja iliyookotwa na Villa katika mchuano huo iliwasaza katika nafasi ya tisa kwa alama 41, tatu zaidi kuliko Arsenal ambao watakuwa wenyeji wa Tottenham Hotspur mnamo Machi 14, 2021, uwanjani Emirates.

Newcastle kwa sasa wameshinda mechi mbili pekee kutokana na 17 zilizopita. Kushindwa kwa mara nyingine kungening’iniza padogo zaidi matumaini yao ya kusalia ligini muhula ujao.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Waqo akaidi tena mwaliko wa PIC

TANZIA: Mwanamuziki Muriithi John Walker afariki baada ya...