• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 12:26 PM
CHOCHEO: Ukijua anachepuka, utafanyaje?

CHOCHEO: Ukijua anachepuka, utafanyaje?

Na BENSON MATHEKA

HARRY alitarajia mkewe Cynthia amkasirikie na kununa alipogundua kwamba alikuwa amekula ufuska na kipusa mwingine.

Badala yake, Cynthia alimchangamkia zaidi kwa kumwandalia burudani murwa chumbani. Baada ya wiki moja alimwambia kwa upole na heshima.

“Darling, ukiona nimelegea kukupakulia asali, nieleze badala ya kutafuta mipango ya kando wanaoweza kuharibu uhusiano wetu. Nakupenda sana na nitafanya kila niwezalo kukupa raha na burudani uridhike”.

Harry alikiri kwamba tangu ale uroda nje ya ndoa, mkewe aliboresha shughuli chumbani japo alitarajia kwamba angemkasirikia alipogundua alikuwa amekula vya pembeni.

“Nilijipeleleza na kujuta kwa kumsaliti. Kama Cynthia hangekuwa mwanamke mwenye hekima, mchepuko ungevuruga ndoa yangu,” asema Harry.

Hali ilikuwa hivyo kwa Dave alipogundua mkewe alikuwa akichepuka na mfanyakazi mwenzake.

“Nilipomuuliza kwa nini anagawa asali, aliniambia kwamba ninafaa kujiuliza nilichokosa hadi akaamua kukitafuta kwa wanaume wengine. Niligundua kuwa sikuwa nikimpa muda wa kutosha na ikabidi nibadilishe tabia,” asema Dave.

Kulingana na ripoti ya shirika la Maisha Mema kuhusu kisa cha Dave, mkewe alifichua kwamba hakuwa akigawa asali japo alikuwa na uhusiano wa karibu na wafanyakazi wenzake wanaume.

“Lakini uhusiano huo ungemfanya ashawishike kuhanya kwa kuwa ilikuwa nadra kuketi na mumewe na kujadili masuala muhimu. Alihisi upweke hadi mumewe alipohisi kulikuwa na hatari ya kupokonywa mkewe na mafisi afisini mwao, akazidisha mapenzi ikiwa ni pamoja na nderemo chumbani na kumpeleka kujivinjari maeneo tofauti,” inasema ripoti iliyoandikwa na mshauri wa wanandoa Trizah Karimi.

Kulingana na mwansaikolojia huyu, kuna watu wanaowachangamkia wachumba wao zaidi wakigundua wanachepuka.

“Ni hatua inayohitaji ukomavu mkubwa ikizingatiwa kuwa kuchepuka ni kosa na usaliti wa hali ya juu ambao mtu anaweza kumfanyia mwenziwe,”asema Trizah na kuongeza kuwa kufanya hivi kunamzuia kuendelea na uhanyaji.

“Sio watu wengi wanaoweza kufanya hivyo lakini wanaozidisha upendo kwa wachumba wao wakigundua wanashiriki mipango ya kando, huwa wanaokoa uhusiano wao wa kimapenzi kuliko wale wanaonuna na kuzua ugomvi,” asema.

Hata hivyo, anasema hili linawezekana anayesalitiwa akigundua na kukubali mapungufu yake katika uhusiano.

“Sio lazima iwe ni kulegea chumbani. Inaweza kuwa lugha unayotumia au marafiki unaojumuika nao. Unaweza kuwa mpishi bora lakini uwe mtu wa kelele na ugomvi,” aeleza Trizah.

Gerald, mwanamume mwenye umri wa miaka 33 na Nekesa mwanadada mwenye umri wa miaka 27 wanasema kwamba waliamua kuhanya, wenzao walipopunguza makeke chumbani. Hata hivyo, Nekesa asema mumewe alipoingiwa na wivu na kuboresha tendo, aliacha tabia hiyo.

“Ilikuwa hatari sana,” asema na anashauri watu watafute mbinu mbadala za kunogesha mapenzi.

Mwansaikolojia Doreen Shigadi wa shirika la Big Hearts Nairobi, anasema kuwa sio watu wengi wanaochangamkia wachumba wahanyaji au wanaoshuku si waaminifu.

“Ni wachache sana hasa wanaume wanaoweza kuwasamehe wenzao wakigundua wanagawa asali nje ya ndoa. Tabia hii imevuruga ndoa na mahusiano ya mapenzi. Hauwezi kusaliti mtu wako na utarajie akuchangamkie roho safi,” asema.

Anashauri watu kuepuka tabia zinazoweza kutumbukiza wachumba wao kwenye majaribu ya ulaghai wa mapenzi.

“Adui mkubwa wa uhusiano wa mapenzi ni mchepuko. Unavunja uhusiano na hata msipotengana, penzi litakuwa limechuja.

Hata hivyo, kuna wanaotambua walichangia tabia ya michepuko na ndio sababu hurekebisha na kuwachangamkia wenzao,” asema Shigadi.

Lily Koech, mwanadada mwenye umri wa miaka 26 na Bonface Wambua mwenye umri wa miaka 35 wanasema hawawezi kuwakumbatia wachumba wao wakigundua wanachuuza asali.

“Siwezi kumkaribia. Hauwezi kunisaliti kwa sababu ya upungufu wangu kisha udai unanipenda,” asema Lily.

You can share this post!

FUNGUKA: ‘Si uchizi, ni raha zangu…’

FATAKI: Ubabe-dume, ujeuri na ujuaji mwingi si ujasiri, ni...