• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 6:47 AM
Uhuru amwomboleza mwanahabari aliyefariki kutokana na corona

Uhuru amwomboleza mwanahabari aliyefariki kutokana na corona

CHARLES WASONGA na PSCU

RAIS Uhuru Kenyatta ametuma risala za rambirambi kwa familia ya mwanahabari Robin Njogu ambaye alifariki Jumatatu usiku baada ya kuugua Covid-19. Marehemu alifariki katika hospitali ya Aga Khan ambako alikuwa amelazwa akipokea matibabu.

Kwenye taarifa ilitolewa na kitengo cha habari za rais (PSCU), Rais Kenyatta alimtaja Njogu kama mwanahabari shupavu ambaye mchango wake katika vitengo vya redio na uanahabari wa mitandaoni umestawisha sekta ya uanahabari na mawasiliano.

Hadi kifo chake, marehemu alikuwa Mhariri Msimamizi wa Habari katika kitengo cha Redio katika Shirika la Habari la Royal Media Services (RMS).

“Robinson alikuwa mwanahabari mwenye tajriba na uzoefu mkubwa ambaye aliwafunza chipukizi wengine katika tasnia ya uanahabari. Daima tutaendelea kuenzi weledi wake, haswa katika kitengo cha redio ambapo alikuwa kielelezo cha ufanisi,” akasema Rais Kenyatta.

Kiongozi wa wa taifa aliongeza kuwa Njogu alikuwa mwanahabari wa kutegemewa zaidi alipohudumu katika kitengo cha habari katika Ikulu kati ya 2013 na 2017.

“Nilifaidi pakubwa katika kutangamana kwangu na Robin wakati ambapo alifanya kazi katika Ikulu pamoja na wanahabari wengine wa kitengo cha habari za rais. Alikuwa mfanyakazi wa kuaminika na kupigiwa mfano,” Rais Kenyatta akasema.

Kwa upande wake Naibu Rais William Ruto alimtaja marehemu Njogu kama mtaalamu aliyependa kazi yake ambayo aliifanya kwa bidii na moyo wa kujitolea.

“Alizingatia maadili ya uanahabari na kutoa mchango wake katika kuendeleza taalamu hii,” Dkt Ruto akasema kwenye taarifa aliyotuma kupitia ukarasa wake wa twitter.corona

Njogu amefariki siku chache tu baada ya kifo cha mama yake.

You can share this post!

Korti yakataa kutupa kesi ya mauaji dhidi ya Babu Owino

HARAMBEE STARS: Mulee atakiwa atembelee kujionea vipaji...