• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 10:55 AM
FAUSTINE NGILA: Tuzime video feki zisivuruge uchaguzi 2022

FAUSTINE NGILA: Tuzime video feki zisivuruge uchaguzi 2022

Na FAUSTINE NGILA

HUENDA hujaziona lakini katika kipindi cha miezi minne iliyopita nimekumbana na video nyingi feki za kisiasa kuwahusu Naibu Rais William Ruto na kiongozi wa ODM, Raila Odinga, zikisambaa mitandaoni.

Ni hali inayotia wasiwasi, kwamba fikra za wapigakura zitatekwa na makusudi ya wanaounda video hizi.Hasa ikizingatiwa kuwa Wakenya wengi huamini chochote kinachochapishwa kwenye mitandao ya kijamii.

Teknolojia inayounda video hizi ni ya kiwango cha juu mno, kwani inawezesha kutoa nakala ya maumbile ya mtu, sauti yake, sura yake, anavyotembea n ahata anavyotabasamu.

Ni video chache tu ambazo utatambua kuwa ni feki, lakini nyingi zimefanywa kwa ustadi mno, na kutia maneno ya uwongo kwa vinywa vya wanasiasa.

Utata zaidi unajitokeza ukitazama mtindo wa siasa humu nchini, ambapo wanasiasa husema mambo fulani lakini wanapokamatwa na serikali kwa kuchochea chuki, wanadai si wao waliyatamka.

Hivyo, bila kuchukua hatua za kiteknolojia kudhibiti video hizi pamoja na wanaoziunda, itakuwa rahisi mno kwa wanasiasa kufoka maneno machafu kisha kisingizia video hizi.

Uwezekano wao kujificha nyuma ya ukuta wa video feki ni tisho kuu kwa amani inayohitajika, hasa katika msimu huu ambapo kampeni za Uchaguzi Mkuu zimeshika kasi.

Tayari wanasiasa 10 wiki iliyopita waliitwa na Tume ya Kitaifa ya Uwiano na Utangamano (NCIC) kueleza sababu zao kutoa matamshi yaliyochochea ghasia kwenye chaguzi ndogo za Machi.

Hii ni ishara kuwa idadi hii huenda ikaongezeka mwaka unavyozidi kukomaa na kura ya 2022 ikijongea.Ingawa Idara Ya Upelelezi wa Jinai (DCI) imekuwa ikifanya kazi nzuri ya kunasa watu wanaoeneza habari feki, itahitaji kuwekeza katika teknolojia za kiwango cha juu zaidi kuweza kutambua video bandia na watu wanaozitengeneza.

Hebu fikiria. Video feki inayomwonyesha Bw Odinga akisema “Ruto tosha” ikisambazwa kwenye mtandao wa kijamii wa Facebook, ambao unakisiwa kutumiwa na Wakenya zaidi ya milioni 7 waliotimu kupiga kura!Au hata video feki inayodai kufichua maovu ambayo Dkt Ruto hufanya nyakati za usiku! Kanda moja tu pekee ya aina hii ikiwafikia Wakenya milioni moja kwenye Twitter au WhatsApp inatosha kubadilisha matokeo ya uchaguzi.

Ni kweli kuwa Wakenya wengi wanamiliki simu za kisasa na wamechangamkia mitandao ya kijamii kuliko mataifa mengine barani Afrika.Hata hivyo, zaidi ya asilimia 80 ya Wakenya hawa hawana ujuzi wa kidijitali kutambua ni ujumbe upi wa ukweli na upi ni feki.

Hata ninapoipa changamoto DCI kunoa makali yake kiteknolojia, wananchi wenyewe wanahitaji kujielimisha kuhusu masuala haya sio tu kutarajia serikali iwahamasishe.Itakulazimu kuweka programu ya kutambua video, picha na sauti feki kwa simu yako usije ukahadaiwa na wakora wa siasa; wanaotumia ujuzi wa kidijitali kuchapisha mambo feki mitandaoni.

Itabidi uwe makini zaidi kupuuza mawasialiano ya aina hii. La sivyo, utanaswa kwenye mtego wa kuamini chochote kinachosambazwa mitandaoni, na huenda hatimaye ukahusika kuchochea chuki na hata ghasia.

You can share this post!

Hofu wanaofariki baada ya kupata chanjo wakiongezeka

Magufuli bado yuko mteja