• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Mtangazaji wa zamani wa NTV afariki kutokana na corona

Mtangazaji wa zamani wa NTV afariki kutokana na corona

NA WANGU KANURI

Aliyekuwa mtangazaji wa habari katika runinga yaNTV Winnie Mukami amefariki. Mukami aliaga dunia Alhamisi baada ya matatizo ya ugonjwa wa Covid-19.

Mnamo 2010, Mukami aliondoka NTV, kampuni inayomilikiwa na Aga-Khan, baada ya kuhudumu kwa miaka saba.

“Nilifurahia sana kipindi ambacho nilikuwa kwenye vyombo vya habari na wakati ambapo kipindi changu kilitamatika, nilikumbatia mabadiliko hayo na nikaanza kufikiria jinsi nitasonga mbele. Sasa mimi ni mwanabiashara aliyejisimamia ambaye anafikiri namna ya kusaidia jamii hata ingawa kufikia hapa haijakuwa kazi rahisi,” alisema wakati huo.

Mukami alijulikana mnamo mwaka wa 2003 wakati ambapo alipeperusha habari za NTV wakati wa uzinduzi wake.

Alianza kazi yake ya uanahabari katika kituo cha KBC kama mwanahabari na mtayarishaji wa redio na televisheni wa masuala ya hivi sasa.

Kifo chake kinatujia siku mbili baada ya kifo cha mwanahabari wa Royal Media Services, Robin Njogu aliyefariki kutokana na ugonjwa huu wa Covid-19.

Wakati ambapo alikuwa akifanya kazi katika Nation Media Group, nyota yake iling’aa na akawa analinganishwa na wanahabari wa ngazi ya juu kama Katherine Kasavuli, Swaleh Mdoe, Sophie Ikenye na Louis Otieno miongoni mwa wengine.

Katika mahojiano ya hapo awali, Mukami alieleza kuwa tukio ambalo anakumbuka sana alipokuwa akifanya kazi katika televisheni ni wakati wa vurugu za baada ya uchaguzi wa mwaka 2007, ambapo alikuwa studioni siku nzima akiripoti uhalisia wa matukio jinsi yalivyochipuka.

Mnamo 2018, aliteuliwa kwenye bodi ya kampuni ya Kenya Pipeline kwa kipindi cha miaka mitatu na aliyekuwa sekretari wa mafuta ya petrol John Munyes. Zaidi ya ushupavu wake kwenye vyombo vya habari na serikali, Mukami alifichua kuwa alikuwa akiuza uji kwa wafanyikazi wa mijengo kabla hajapata uajiri rasmi.

Winnie Mukami alieleza uchapishaji huo kuwa angezunguka mtaa wa Kitengela akitafuta mahali ambapo ujenzi ulikuwa ukifanywa na kuuza uji wake. Aliyatumia mapato ya biashara hiyo kuwasaidia wazazi wake na ndugu zake watatu.

You can share this post!

Kifo cha Magufuli chamletea Harmonize dhiki kuu

Mwalimu taabani kwa kumdhulumu mtahiniwa wa KCSE