• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 6:21 PM
IEBC yasaka ardhi kuhamisha makao

IEBC yasaka ardhi kuhamisha makao

Na PATRICK LANG’AT

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imetangaza mpango wa kuhamisha afisi zake hadi nje ya jiji ili kuzuia mali yake kuharibiwa wakati wa maandamano ya kupinga matokeo ya uchaguzi siku zijazo.

IEBC ina afisi zake katikati mwa jiji la Nairobi katika jengo la Anniversary Towers karibu na Chuo Kikuu cha Nairobi na sasa inapendekeza ihamishie makao yake kwenye ekari tano ya ardhi kilomita 20 nje ya jiji ili kuzuia hasara iliyotokea mwaka wa 2017.

Jengo hilo limekuwa makao makuu ya IEBC kwa muda wa miaka 13.

“Ardhi tunayoazimia kuhamia itakuwa kilomita 20 kutoka katikati mwa jiji na itakuwa ekari tano. Pia lazima iwe inaweza kufikiwa kwa urahisi kupitia barabara zilizotengenezwa vizuri.

“Pia lazima iwe na hatimiliki yake na iwapo imekodishwa basi lazima iwe imesalia chini ya miaka 60 kabla ya muda huo kukamilika,” ikasema IEBC kwenye taarifa ya zabuni katika magazeti ya hapa nchini mnamo Machi 16.

Tangazo hilo lilitiwa saini na kaimu Afisa Mkuu Mtendaji Hussein Marjan. Wale ambao wana ardhi na wanataka kuiuzia IEBC wamepewa hadi Machi 30 ili kuwasilisha fomu zilizojazwa.

“Tume itaendelea kutafuta pesa za kuhakikisha kuwa inafadhili mradi huo. Afisi za sasa ziko katika jengo ambalo lina afisi nyingine pia na lina msongamano mkubwa. Hii huzua changamoto kubwa hasa wakati wa uchaguzi ambapo shughuli huwa nyingi,” akasema Mwenyekiti wa IEBC, Bw Wafula Chebukati alipofika mbele ya kamati ya bunge kutoa ripoti ya kila mwaka ya matumizi ya fedha za tume hiyo.

IEBC imekuwa ikilipa kodi ya Sh100 milioni kila mwaka na kiasi hicho hakijumuishi fedha zinazotumika kuandaa mafunzo kwa wafanyakazi wa tume hiyo pamoja na mikutano mingine.

“Kupatikana kwa ardhi hiyo na kujengwa kwa afisi mpya kutasaidia tume kupunguza gharama zake hasa katika ulipaji kodi na kukodisha maeneo ya kufanyia mikutano na kuandaa mafunzo kwa wafanyakazi wake. Pia kutakuwa na nafasi za kutosha kuhifadhi vifaa vyake,” akasema Bw Chebukati mnamo 2018, wazo hilo lilipokumbatiwa.

Mnamo 2016, kinara wa ODM, bW Raila Odinga aliongoza wafuasi wake kuandaa maandamano karibu na afisi hizo wakimtaka aliyekuwa mwenyekiti wa IEBC, Issack Hassan abanduke, wakidai hakuwa na uwazi katika kuandaa uchaguzi mkuu wa 2017.

Ripoti ya Muungano wa Wafanyabiashara wa Sekta ya Kibinafsi (KEPSA) ilisema zaidi ya Sh120 milioni zilipotea wakati wa maandamano hayo huku zaidi ya biashara 500 zikivurugwa na kufungwa wakati huo.

Mnamo 2017, mbunge wa Starehe, Bw Charles Njagua alitaka IEBC iondoe makao yake makuu katika jengo la Anniversary Towers ambalo liko katika eneobunge lake.

You can share this post!

Kizaazaa Jaji kulalama faili ya kesi ya Bobi Wine imetoweka

Mipango kufanya Raila apate urais raundi ya kwanza