• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 12:45 AM
Chama cha Ruto chaaibishwa uchaguzini Machakos

Chama cha Ruto chaaibishwa uchaguzini Machakos

Na PIUS MAUNDU

USHINDI wa Bi Agnes Kavindu Muthama kwenye uchaguzi wa useneta, Machakos Ijumaa umechukuliwa na wafuasi wa chama cha Wiper kuwa pigo kwa juhudi za Naibu Rais William Ruto kujipenyeza kwenye ngome hiyo.

Bi Kavindu alizoa kura 104,352 huku Bw Urbanus Muthama Ngengele wa chama cha United Democratic Alliance (UDA) akiambulia kura 19,726 pekee.

Mbunge wa Mavoko Patrick Makau alisema chama cha UDA kinachohusishwa na Naibu Rais, kimejifunza kuwa siasa si mchezo wa watoto.

“Chama cha UDA kilikufa siku kilizaliwa Ukambani. Nawashauri wanachama wake waungane na kinara wetu Bw Kalonzo Musyoka tunapoelekea Uchaguzi Mkuu wa 2022,” akasema Bw Makau katika kituo kikuu cha kujumuisha matokeo, Machakos Academy.

Bw Ngengele aliyekubali kushindwa, alitetea kura alizopata ikizingatiwa chama alichotumia.

“Chama cha UDA ni kipya Ukambani. Kupata karibu kura 20,000 si jambo dogo. Tutasonga mbele na juhudi za kujiimarisha,” akasema.

Kwingineko, Mbunge wa Mwala, Bw Vincent Musyoka aliyekuwa miongoni mwa waliompigia debe Bw Ngengele, alidai chama cha UDA kimeonyesha kuwa kinaweza kumaliza umaarufu wa Bw Kalonzo.

Msimamizi wa uchaguzi huo Bi Joyce Wamalwa, aliwahimiza wanasiasa wafanye kampeni za kuwavutia wapigakura wajitokeze kwa wingi siku za uchaguzi.

Kati ya wapigakura 623, 536 waliosajiliwa, ni 131, 940 pekee waliojiteza na kushiriki kwenye uchaguzi huo.

Kwenye hotuba ya kukubali ushindi wake, Bi Kavindu aliwataka wafuasi wake waache kumchokoza mwenyekiti wa chama cha UDA, Bw Johnson Muthama, akisema ni mzazi mwenzake na yafaa aheshimiwe.

You can share this post!

Mipango kufanya Raila apate urais raundi ya kwanza

Kufeli sekondari hakukumzuia kuwa Rais