• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
WALLAH BIN WALLAH: Tumia Kiswahili kujinyanyua kimaisha, usilaze damu aisee!

WALLAH BIN WALLAH: Tumia Kiswahili kujinyanyua kimaisha, usilaze damu aisee!

NA WALLAH BIN WALLAH

KILA kitu kinatafutwa papa hapa duniani. Ukikosa kukipata unachokitaka, usiseme hakipo au hakipatikani ama kimekosekana! Aliyekosa kukipata ni wewe!

Au labda unacho lakini hujui kukitumia kikuletee faida! Kauli hiyo inanikumbusha hotuba na nasaha zilizotolewa katika Kongamano la Kiswahili lililoandaliwa na Mkurugenzi wa Nurisha Africa, Mwalimu Titus Sakwa kwa udhamini wa Shirika la Uchapishaji Vitabu la East African Educational Publishers; kwa hisani ya Meneja Mchapishaji, Ndugu Job Mokaya, jijini Nairobi siku ya Jumamosi tarehe 13, Machi 2021.

Kongamano hilo babu kubwa lilihudhuriwa na wapenzi wa Kiswahili kutoka janibu zote za Kenya. Baadhi ya mabingwa wa Kiswahili waliohudhuria ni Balozi Arthur Andambi, Mwalimu Yassin kutoka Garissa, Mwalimu K.M. Anduvate, Estrada Bin Estrada kutoka Kwale, Yusufu Sultane kutoka Kajiado, Eric Muteti wa Nairobi na wengineo.

Walumbi wakuu waliohutubia kutoa wasia na nasaha kwa waungwana wasikivu ni Dada Zubeda Koome, Ndugu Nuhu Bahari, Ndugu Hassan mwana wa Ali, Dkt Hamisi Babusa, Ndugu Job Mokaya, Mwalimu Abubakar Tsalwa, Mwalimu Titus Sakwa, Balozi Arthur Andambi, Mwalimu Wallah Bin Wallah na wengineo.

Katika ukumbi nadhifu uliopambwa ukapambika, wapenzi wa Kiswahili waliovaa nyuso changamfu zilizovishwa vitamvua au barakoa za kudhibiti virusi vya korona, awali walikaribishwa kwa burudani za mashairi na maonyesho anuai yaliyofuatiwa na kuzinduliwa rasmi vitabu viwili ambavyo ni Malenga wa Ziwa Kuu , kitabu chenye mashairi mazuri yasiyo kifani kilichoandikwa na Wallah Bin Wallah miaka mingi iliyopita.

Katika diwani hiyo Malenga wa Ziwa Kuu ndimo utakamopata mashairi kama yale: Kilio si Dawa , Nimpe Mama Zawàdi Gani ?, Kiswahili Nairobi , Kufu ya Umalenga pamoja na shairi lake lile maarufu Kiswahili Kitukuzwe alilolitunga alipokuwa mwanafunzi wa kidato cha pili. Kitabu kingine kilichozinduliwa ni Picha ya Karne kilichoandikwa na Hassan mwana wa Ali.

Wawasilishaji wakuu walipokuwa wakitoa nasaha waliwahimiza na kuwakumbusha wasikilizaji wazingatie kwamba Kiswahili ni bidhaa adhimu sana inayostahili na kustahiki kuuzwa ghali zaidi. Ndugu Nuhu Bahari aliwatanabahisha wapenzi wa Kiswahili kwamba “Lugha ya Kiswahili ni utajiri, ni pesa, ni ajira, ni bidhaa adhimu na adimu kama dhahabu!

Anzeni leo kubidhaisha Kiswahili kwa kuandika makala, mashairi na vitabu mkauze! Fanyeni tafsiri na ukalimani! Tazameni wataalam ambao wameajiriwa kama vile walimu wa Kiswahili, watangazaji, wahariri na waandishi wa habari, wanalipwa pesa lukuki kwa sababu ya Kiswahili!”

Ndugu wapenzi, tumia Kiswahili upate pesa! Ukishindwa usiseme pesa hakuna! Kiswahili ni bidhaa ya kuleta pesa! Ukikosa kutumia Kiswahili umejikosesha wewe mwenyewe kupata pesa, usiseme zimekosekana! Uza Kiswahili upate pesa!!!!!

You can share this post!

Corona ilivyomsaidia kuvuta wateja wa nyama

GWIJI WA WIKI: DKT EVANS MAKHULO