• Nairobi
  • Last Updated March 18th, 2024 8:55 PM
Wanasiasa wa Mlima Kenya walia ‘kunyanyaswa’ na rais

Wanasiasa wa Mlima Kenya walia ‘kunyanyaswa’ na rais

Na JAMES MURIMI

BAADHI ya viongozi wa kisiasa kutoka eneo la Kati wamelalamika kuwa Rais Uhuru Kenyatta anazima vyama vidogo vya kisiasa eneo hilo.

Viongozi hao wamemtaka rais kupatia vyama vya kisiasa vinavyoibuka eneo hilo nafasi ya kustawi.

Aliyekuwa Waziri wa Kilimo, Mwangi Kiunjuri na Mwakilishi wa Wanawake katika Kaunti ya Laikipia, Cate Waruguru waliungana kumtaka Rais Kenyatta kukuza demokrasia katika eneo hilo.

Wawili hao walionekana kuzika tofauti zao za kisiasa kwa kuitisha kikao cha pamoja na wanahabari, ambapo waliitaka serikali isaidie kukuza vyama vya kisiasa vyenye mizizi ya eneo hilo.

“Kama watu wa eneo la Kati ya Kenya, hatuogopi kutoa malalamishi yetu na kutetea vyama vya kisiasa tulivyo navyo. Tunamuomba Rais Kenyatta aturuhusu tujipange kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka ujao,” alisema Bi Waruguru.

“Maeneo mengine yanafurahia demokrasia, lakini katika Mlima Kenya tumelemazwa. Tunataka demokrasia kuhusu siasa za eneo,” aliongeza.

“Iwapo demokrasia haitahakikishwa na rais, basi eneo la Kati ya Kenya litaendelea kutazama maeneo mengine yakitawala siasa za kitaifa,” alisema Bi Waruguru.

Bw Kiunjuri, ambaye ni kiongozi wa The Service Party, alisema vyama vinavyoibuka katika eneo hilo vinakadamizwa na Jubilee kwa kunyimwa haki ya kufurahia demokrasia.

You can share this post!

Ufisadi wavunja raia moyo wa kulipa ushuru – TI

Wakenya waendea medali za dhahabu ndondi za Ukanda wa Tatu...