• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 10:10 AM
Sossion aililia serikali shule zifunguliwe Mei

Sossion aililia serikali shule zifunguliwe Mei

Na CHARLES WASONGA

KATIBU Mkuu wa Chama cha Kitaifa cha Walimu (Knut) Wilson Sossion ameiomba serikali kuruhusu kufunguliwa kwa shule mnamo Mei 10, ilivyoratibiwa licha ya serikali kuweka masharti mapya ya kudhibiti msambao wa corona.

Akiongea Jumatatu asubuhi katika runinga ya Citizen TV Bw Sossion alisema kalenda ya masomo iliyotangazwa na Wizara ya Elimu Desemba, 2020 haifai kuvurugwa na vikwazo vipya vilivyotangazwa na Rais Uhuru Kenyatta kuzuia maambukizi ya Covid-19.

“Tunaomba serikali kuweka mipango itakayohakikisha kuwa utaratibu wa masomo hautavurugwa tena. Tunahimiza kwamba kufikia Mei walimu watakuwa wamepewa chanjo na shule kufunguliwa. Hatutaki watoto kukaa nyumbani kwa muda mrefu zaidi kama ilivyokuwa mwaka jana ambapo wengine waliathirika pakubwa,”akasema.

“Hata ikiwezekana likizo ya wakati huu inafaa kufupishwa ili watoto warejee shuleni ili watoto wasiathirike na maovu ya kijamii yanayosababishwa na marufuku dhidi ya corona,” Bw Sossion ambaye pia ni Mbunge Maalum wa chama cha ODM.

Katibu huyo Mkuu wa Knut alielezea matumaini kuwa kufikia mwezi Mei, serikali itakuwa imelegeza masharti ya kudhibiti corona iliyoweka juzi kabla ya tarehe ambayo shule zinapaswa kufunguliwa.

Mnamo Ijumaa, Rais Uhuru Kenyatta alitoa maagizo mapya na makali ya kuzuia msambao wa corona ambapo aliamuru kusitishwa kwa masomo katika taasisi zote za masomo nchini.

Aidha, aliweka marufuku ya watu kuingia na kuondoka kaunti tano ambazo zimeshuhudia idadi ya juu ya maambukizo ya corona, miongoni mwa masharti mengine. Kaunti hizo ni Nairobi, Machakos, Kiambu, Kajiado na Nakuru.

You can share this post!

Mwanamke mwenye ndevu asimulia jinsi alivyojikubali

Aina hatari ya corona imetua nchini – Kagwe