• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 6:55 AM
Droni ya jirani yamtia hofu mke wa Ruto

Droni ya jirani yamtia hofu mke wa Ruto

Na MARY WAMBUI

POLISI Jumanne walimhoji raia wa Uingereza ambaye mtambo wake wa kupiga picha angani (droni) ulipaa katika eneo la nyumba ya Naibu Rais, Dkt William Ruto katika mtaa wa Karen, Nairobi.

Kulingana na Kamanda Mkuu wa Polisi eneo la Nairobi, Bw Augustine Nthumbi, droni hiyo ya Bw Hind Jeremy, 37, ilisababisha hofu ilipoonekana na mkewe Naibu Rais, Bi Rachel Ruto.

“Bi Ruto alisema alikuwa ndani ya nyumba mwendo wa saa tisa alasiri siku ya Jumatatu, alipoona kifaa hicho kikipaa kwenye boma lao kutoka kwa Mwingereza huyo ambaye wanapakana naye,” akasema Bw Nthumbi.

Polisi walifika katika nyumba hiyo ya Dkt Ruto na kuchukua kifaa hicho, kabla ya kumwita Mwingereza huyo kwa mahojiano.

Bw Nthumbi alisema kuwa uchambuzi unafanywa ili kujua yaliyomo kwenye droni hiyo.

“Mtambo huo wa droni haujakuwa na kiambatisho chochote cha kutia wasiwasi kulingana na uchunguzi wa awali. Hata hivyo, tulichukua kadi iliyokuwa ndani ili tujue walikuwa wakipiga picha za aina gani na kwa lengo lipi,” alisema Bw Nthumbi.

Kulingana na ripoti, wageni waliokuwa wamemtembelea mwanume huyo ndio waliobeba mtambo huo, waipige picha nyumba yake na kisha wampe kifaa hicho kama zawadi.

Kisa hicho bado kinafanyiwa uchunguzi zaidi na Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) Nairobi, Kitengo cha Polisi cha kupambana na Ugaidi (ATPU) na Huduma ya Kitaifa ya Uchunguzi pamoja na mamlaka ya Safari za Angani.

You can share this post!

KCSE: Afisa abambwa na Magoha akisaidia watahiniwa kwa...

Obado afufua mashambulizi dhidi ya Raila