Na SAMMY WAWERU
MBUNGE wa Kiambaa Bw Paul Koinange amefariki Jumatano. Familia yake imesema amefariki kutokana na makali ya virusi vya corona, katika hospitali moja jijini Nairobi ambapo alikuwa anapokea matibabu.
Bw Koinange alikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama Bungeni.
Kwenye salamu za pole kwa familia yake, jamaa, marafiki na wakazi wa Kiambaa, Rais Uhuru Kenyatta ameongoza taifa kumuomboleza mbunge huyo akisema Kenya imepoteza kiongozi aliyejitolea kusaidia kuimarisha usalama wa nchi.
“Kifo kimetupokonya kiongozi shupavu na mkakamavu. Kiongozi ambaye lengo lake lilikuwa kuimarisha usalama wa nchi, utulivu na maendeleo,” akaelezea Rais Kenyatta akimuomboleza mbunge huyo kupitia taarifa yake kwa vyombo vya habari.
Alichaguliwa kuingia bungeni 2017, kwa tiketi ya chama tawala cha Jubilee.