• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 1:08 PM
Hii kafyu inaumiza wananchi – Kalonzo

Hii kafyu inaumiza wananchi – Kalonzo

Na MWANGI MUIRURI

KINARA wa Wiper Democratic Movement amemtaka Rais Uhuru Kenyatta awajibikie utathimini upya kwa upana mikakati aliyoweka Ijumaa katika Kauntio tano akilenga kuzima makali ya Covid-19, akiitaja kuwa hasi.

Kaunti hizo ni Machakos, Nairobi, Nakuru, Kajiado na Kiambu zilizozimwa kutangamana na wengine katika Kaunti zingine 42 huku wakipewa ruhusa ya kutembea tu ndani ya mduara huo wa majimbo matano.

Bw Kalonzo alisema kuwa Rais anafaa kuelewa kuwa kuweka kafiu ya kuanzia saa mbili usiku haizingatii hali halisi ya maisha ya Wananchi wa kawaida ndani ya Kaunti hizo.

Alisema kuwa wengi katika Kaunti hizo wakifunga kazi saa kumi na moja jioni hufika kwa steji za uchukuzi wa wanakoishi mwendo wa saa kumi na mbili kisha wanangoja matatu hadi saa 12 na nusu na hatimaye msongamano wa magari unawaweka kwa barabara hadi saa mbili usiku na ina maana kuwa “unawagonganisha na maafisa wa polisi ukiwaambia wawe ndani ya nyumba saa mbili usiku.”

Alisema kuwa hakuna uchukuzi wa moja kwa moja ambao utakuweka ndani ya nyumba yako na hata madereva na makanga wa hayo magari ya uchukuzi watatatizika pakubwa wakijaribu kurejea makwao baada ya kuwasafirisha abiria katika hali hiyo.

Alisema kuwa kafyu hiyo inafaa kiusongeshwa hadi saa nne za usiku na pia kuwe na mikakati pana ya kuwapiga jeki wananchi ambao katika kaunti hizo watapoteza riziki.

“Baa zimefungwa sambamba na makanisa. Kuna kazi zimepotea na pia wanaotegemea watakaochunjwa kutoka ajira. Ni lazima kuwe na mikakati ya kuwapa kiinua mgongo kwa kuwa Katiba yetu inawapa haki ya maisha yasiyo na mahangaiko,” akasema.

Aidha, alisema kuwa raia katika kaunti hizo tano watakabiliwa na mfumko wa bei kufuatia kuzimwa kwa uchukuzi kutoka maeneo mengine hivyo basi kutatiza kupatikana kwa bidhaa muhimu sokoni hasa za kilimo.

Aidha, alisema kuwa rais anafaa kuamrisha upimaji wa halaiki kwa wenyeji katika kaunti hizo ili walio wagonjwa watambulike haraka na mapema kabla hawajasambaza virusi hivyo kwa wengine, na watibiwe bila kutozwa malipo kwa kuwa hili ni janga la kitaifa.

Aliosema kuwa Serikali inaonekana kutokuwa na sera maalum ya kupambana na janga la Covid-19 akisema kuwa hata chanjo yenyewe haina ile dharura inayofaa, huku pia kukiwa na ya mabwanyenye na ambayo inasemwa kuwa na uhakika wa utendakazi wa asilimia 91 huku ya walala hoi ikiwa na uhakika wa asilimia 76.

Bw Kalonzo alisema kuwa chanjo hiyo ya uhakika wa juu ikiuzwa kati ya Sh8, 000 na Sh11, 000 ina maana kuwa haitawezekana kufikiwa na masikini wa taifa hili hivyo basi kuzua mgawanyiko wa Wakenya kwa msingi wa hadhi katika haki ya kuafikia afya bora.

Alisema kuwa janga hili linafaa kuwa limethibitiwa kabla ya mwezi Mei kufika.

You can share this post!

Koinange alikuwa kiongozi wa kuaminika, UhuRuto...

SULUHU APATA MPANGO TZ