• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 3:03 PM
Hesabu za Uhuru 2022 zamkosesha usingizi

Hesabu za Uhuru 2022 zamkosesha usingizi

Na MWANGI MUIRURI

RAIS Uhuru Kenyatta ako na kibarua kigumu cha kujipa ushawishi wa kuamua mwelekeo wa urithi wa 2022 huku akisukumwa na mirengo minne ya kisiasa.

Mrengo wa kwanza unahusu wandani wake ambao wameweka ajenda wazi kuwa wangependelea urithi huo umwendee kinara wa ODM Bw Raila Odinga. Nao mtandao wa familia pana ya mwanzilishi wa taifa hayati Mzee Jomo Kenyatta ambaye ni babake rais Uhuru nao ukisemwa kuwa unampendela Seneta wa Baringo Bw Gideon Moi aibuke kuwa rais wa tano baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.

Wengine ndani ya baraza la mawaziri nao wametangaza wazi kuwa wanampendelea Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiang’i.

Nao wapiga kura wengi wa ngome ya rais ya Mlima Kenya iliyo na nguvu ya ujumla wa kura 8 milioni ambazo kila mrengo wa siasa unachumbia kwa udadisi kuwa ndizo zitaamua mshindi wakisemwa kuwa wanampendelea Naibu wa Rais Dkt William Ruto.

“Hii ni mitandao iliyo na nguvu sana na huenda Rais ajipate katika hali sawa na mchezaji kamari ambaye mkononi ako na kadi za kupoteza,” asema Mchanganuzi wa siasa za eneo hilo Prof Ngugi Njoroge.

Kwa mujibu wa aliyekuwa mbunge wa Dagorretti Kusini Bw Dennis Waweru “kunao wanaosema kuwa Bw Odinga hawezi akachaguliwa. Huo ni uongo kwa kuwa Bw Odinga ni Mkenya aliye na nafasi sawa ya kuchaguliwa hata na watu wa Mlima Kenya.” Ni wazo ambalo linaungwa mkono na mbunge wa Gatanga Bw Nduati Ngugi anayesema kuwa “Bw Odinga ako na uwezo wa kumrithi rais Kenyatta.

Aliyekuwa mbunge wa Maragua Bw Elias Mbau aliambia Taifa Jumapili kuwa “kile tu Bw Odinga anahitaji ni wale mabwanyenye na washirikishi wa njama za kumfaa mwaniaji wa Mlima Kenya katika ushindani wa urais wasusie kumhujumu Bw Odinga.”

Anasema kuwa harakati za mabwanyenye hao ndizo zimekuwa pingamizi kuu kwa Bw Odinga kuibuka na ushindi wa kutambulika, akikiri kuwa “kuna mara mbili ambapo Bw Odinga ametushinda (2007 na 2013) lakini ushawishi huo ukatumika kumzima kimabavu kupitia hila na njama.”

Bw Mbau anasema kuwa rais Kenyatta kwa wakati huu anaandaa njama ya uwaniaji wa Bw Odinga akiwa na aliyekuwa mbunge wa Gatanga Bw Peter Kenneth kama mgombezi mwenza na hatimaye nyadhifa zinazoundwa katika ripoti ya BBI zitumike kuwaleta pamoja wengine walio na ushawishi kutoka jamii za Kalenjin, Abaluhya na Wakamba ndani ya muungano huo ndio uwe na makali ya ushindani.

“Hatimaye, Bw Odinga aungwe mkono na mabwanyenye na mtandao wao wa ushawishi ndio akishinda, asihujumiwe kama ilivyo kawaida,” akasema Bw Mbau.

Njama hiyo ikiandaliwa, nao mtandao katika familia ya Kenyatta unachora jinsi urithi huo utamwendea Bw Moi.

“Familia ya hayati Kenyatta iko na heshima kuu kwa familia ya rais wa pili wa taifa hili Marehemu Daniel Moi. Ni mzee Moi ambaye alichangia pakubwa kumthibiti Bw Uhuru Kenyatta alipokuwa katika njia ya kutojielewa kijamii na kimaisha na akamwongoza hadi akamweka katika mkondo wa kushinda urais. Familia hii inapanga njama kali ya kurejesha mkono kupitia nayo kumuunga mkono mwana wa marehemu Moi na ambaye ni Seneta wa Baringo,” akadokezea Taifa Jumapili mmoja wa wandani katika njama hii.

Kwa upande mwingine, ndani ya baraza la mawaziri kumeibuka mtandao ambao umeamua kuasi msimamo wa rais na familia yake na kichinichini kuzindua mradi wa jinsi mmoja wao katika baraza hilo atatuzwa urithi wa Ikulu 2022.

Mnamo Alhamisi katika Mji wa Kangari ulioko Kaunti ya Murang’a, Waziri wa Uchukuzi Bw James Macharia alitangaza kuwa “sisi ndani ya baraza la mawaziri tumeamua huyu Dkt Matiang’i ndiye chaguo letu na tumefika ile awamu ambayo hatufichi nia yetu.”

Itakumbukwa kuwa wiki jana wandani wa Bw Odinga ambao ni Seneta wa Siasa Bw James Orengo na Mbunge wa Suna Mashariki Bw Junet Mohammed walilia kuwa “ndani ya serikali kuna mtandao ambao unaongozwa na Katibu maalum wa Usalama wa Ndani Dkt Karanja Kibicho na unapanga njama ya kumsaliti Bw Odinga na kuteka nyara miradi ya BBI na urithi wa 2022.”

Bw Macharia akiandamana na Dkt Matiang’i, Waziri wa Habari na Teknolojia Joe Mucheru na Naibu wa waziri wa Spoti Bw Zack Kinuthia alitangaza kuwa “sisi haja yetu ni kumpa uongozi wa taifa hili mtu ambaye ataelewa kuhusu miradi tele ambayo tumezindua na ndio isikwame rais Kenyatta akistaafu. Mwenye tumetambua ako na uwezo huo ni Dkt Matiang’i.”

Hayo yakizidi, kura za mashirika ya kibinafsi na pia ile fiche ya utathimini wa usalama wa kisiasa katika kitengo cha Ujasusi zinazidi kuonyesha kuwa Dkt Ruto ndiye ako na guu mbele Mlima Kenya katika ushindani wa urais.

“Ni juu ya rais sasa kuelewa kuwa ako na kibarua na akome ule mtindo wake wa kutoa vitisho kuwa atakuwa na usemi na atashangaza kupitia chaguo lake. La busara sasa ni awajibikie kumaliza awamu yake ya uongozi na atuachie sisi hapa nyanjani tukarangane hadi tuamuliwe na raia kupitia kura na kusiwe na wa kujaribu kumhujumu mwingine,” akasema Bw Rigathi Gachagua, mwandani wa Dkt Ruto.

[email protected]

You can share this post!

Kilichomng’oa Sheffie Weru kazini chapata shahidi...

Ukeketeji Mlima Kenya unavyochochewa na laana