• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
Upanuzi wa uwanja wa ndege wa Manda waanza

Upanuzi wa uwanja wa ndege wa Manda waanza

NA KALUME KAZUNGU

HALMASHAURI ya Usimamizi wa Viwanja vya Ndege nchini (KAA) limeanzisha ukarabati wa uwanja wa ndege wa Manda, Kaunti ya Lamu unaokadiriwa kugharimu serikali kima cha Sh 200 milioni.

Mradi huo ambao unahusisha ujenzi na upanuzi wa njia pamoja na mahali pa kupakisha ndege punde zinapotua umepangwa kuchukua muda wa miezi sita kukamilika.

Mkurugenzi wa KAA Ukanda wa Pwani, Peter Wafula, alisema shughuli ya ujenzi na upanuzi wa sehemu hizo za uwanja wa ndege wa Manda inaendelea baada ya kuanza rasmi mwezi Machi mwaka huu.

Bw Wafula alisema wanatarajia shughuli hiyo ya ujenzi kufikia kikomo ifikapo Agosti mwaka huu.

Afisa huyo alisema KAA iliafikia kupanua na kujenga sehemu husika ili kuwezesha ndege zaidi kutua na kupata nafasi ya kupaki kwenye uwanja huo kwa wakati mmoja.

Alisema sehemu zinazokarabatiwa kwa miaka kadhaa zimekuwa katika hali mbaya, hatua ambayo ilichangia baadhi ya kampuni za usafiri wa ndege nchini, ikiwemo Jambojet kukatiza safari zake kwenye eneo la Lamu.

Bw Wafula anasema anaamini kukamilika kwa ukarabati unaoendelea uwanjani humo kutasaidia kuvutia kampuni nyingi zaidi za ndege kuanzisha huduma zake za usafiri Lamu.

Ujenzi ukiendelea kwenye uwanja wa ndege wa Manda, Kaunti ya Lamu. Jumla ya Sh 200 milioni zimepangwa kutumika kwenye mradi huo. PICHA/ KALUME KAZUNGU

“Tumeanzisha ujenzi na upanuzi wa sehemu za kuegesha na kupaa kwa ndege uwanjani Manda, Kaunti ya Lamu. Sehemu zinazojengwa zilikuwa katika hali duni. Mradi umepangwa kutekelezwa kwa muda wa miezi sita. Shughuli zilianza Machi. Kufikia Agosti kila kitu kitakuwa tayari,” akasema Bw Wafula.

Hatua ya KAA ya kukarabati na kupanua kiwanja cha ndege cha Manda imepokelewa vyema na wadau wa utalii,wawekezaji na wasafiri eneo hilo.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wawekezaji katika sekta ya Utalii, Kaunti ya Lamu, Abdallah Fadhil alipongeza KAA kwa hatua hiyo, akiitaja kuwa yenye natija tele kwa sekta ya utalii Lamu.

“Nimefurahi kwamba KAA imeafikia kukarabati na kupanua kiwanja cha ndege cha Manda. Hii inamaanisha punde shughuli ikikamilika, kampuni nyingi zaidi za ndege zitaanzisha safari zake Lamu. Tutashuhudia watalii wakiingia hapa kwa wingi, hivyo kunogesha sekta hiyo muhimu,” akasema Bw Fadhil.

Mmoja wa wasafiri, Hussein Shukri pia alipongeza ukarabati na upanuzi unaoendelea wa kiwanja hicho cha ndege cha Manda, akisema hatua hiyo itaondoa woga miongoni mwa wasafiri kila wakati ndege zinapotua na kupaa kwenye uwanja huo ambao ulikuwa umesheheni miteremko na mabonde.

Naye Meneja wa Usimamizi na Maendeleo ya Bandari ya Lamu (Lasset), tawi la Lamu, Salim Bunu alisema ujenzi na upanuzi wa uwanja huo wa ndege wa Manda umejiri kwa wakati ufaao ambapo bandari ya Lamu iko kwenye harakati za kuzindua shughuli zake eneo hilo kufikia mwezi Juni mwaka huu.

“Lapsset itakapoanza kufanya kazi itaongeza idadi ya watu eneo hili ambao wengine watakuwa ni wafanyikazi. Wote hao watahitaji usafiri, iwe ni kwa ndege au gari,” akasema Bw Bunu.

You can share this post!

Wakazi wa Pwani kuhamishiwa bara

Mpango wa Raila, Ruto kuungana wapata pingamizi