• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
Wanabiashara wapigia debe chama cha Pwani

Wanabiashara wapigia debe chama cha Pwani

Na SIAGO CECE

MPANGO wa wanasisasa wa Pwani kuzindua chama cha eneo hilo umepigwa jeki baada ya wafanyabiashara wa eneo hilo kuuunga mkono hatua hiyo.

Hata hivyo, wafanyabiashara hao wanawataka wanasiasa wahakikishe kwamba chama hicho kina sura ya kitaifa, ili kivutie wapigakura wengine kutoka sehemu zote nchini.

Mazungumzo yao yanajiri wakati magavana watatu wa Pwani – Hassan Joho (Mombasa), Salim Mvurya (Kwale) na Amason Kingi (Kilifi) – wakikutana majuzi kujadili kuhusu, kinachodaiwa kuwa mipango ya kuunda chama cha Pwani.

Magavana hao watatu wiki jana walikutana na Rais Uhuru Kenyatta, baada ya hapo Jumanne wakakutana katika ofisi za Gavana wa kaunti ya Kwale, licha ya kuwa na tofauti zao za kisiasa hapo awali.

Wakizungumza eneo la Nyali, wafanyabiashra hao wakiongozwa na Fransisca Kitese, walisema lengo lao ni kuwa na usawa katika siasa za eneo la Pwani na nchini nzima.

“Utafiti wetu uligundua kuwa kabila kubwa zaidi hapa Mombasa ni Wakamba, wakifuatiwa na Wamijikenda, GEMA, Waluhya, Wajaluo kisha Waswahili. Licha ya haya, hakuna mbunge yeyote ambaye ametoka katika kabila ambazo si Waswahili au Wamijikenda,” Bi Kitese alisema.

Alisema kabila nyingi za ‘Wabara’ zimebaguliwa kisiasa licha ya wao kuchangia pakubwa katika uchumi wa Pwani.

Kulingana na mkuu wa jamii ya GEMA Mombasa Crispus Waithaka, wafanyabiashara hao wanashinikiza umoja na ushirikiano kati ya makabila yote ambayo yanayoishi Pwani. Hii ni kwa azma ya kukabiliana na ubaguzi hasa katika uongozi.

“Tunakabiliwa na ubaguzi mwingi na watoto wetu hawazingatiwi katika kupata fursa kwa sababu ya majina yao ambayo si ya Kipwani. Tungependa kushirikiana nao katika hicho chama ili kupunguza ubaguzi kama wa rangi au kabila, ” alisema Bw Waithaka.

Aliongeza kuwa licha ya kuwa wazaliwa wa mkoa huo, wakazi wengi wa Mombasa wamenyang’anywa viti vya kisiasa wakati wa uchaguzi na anataka kujiunga na chama hicho cha Pwani katika uchaguzi mkuu wa 2022.

Hata hivyo, Millicent Odhiambo ambaye ni mkazi na mmoja wa wafanyibiashara hao aliomba kuwa wakati chama cha Pwani kitakapozinduliwa, kiungane na muungano wa ‘One Kenya Alliance’ wa Kalonzo Musyoka, Musalia Mudavadi, Gideon Moi na Moses Wetang’ula.

“Yeyote ambaye hatajiunga na muungano wa OKA ana maslahi ya kibinafsi. Tungependa watu waje pamoja na kumaliza ukabila ili tusiwe na mgawanyiko au vita nchini,” alieleza Bi Odhiambo.

Wakati msimu wa siasa unakaribia, viongozi tofauti nchini wanatengeza miungano ili kuhakisha wamefaulu katika kugombea viti vya uongozi.

You can share this post!

Mpango wa Raila, Ruto kuungana wapata pingamizi

Hatimaye serikali yaungama chanjo ya AstraZeneca ina madhara