• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 6:27 PM
JAMVI: ODM inacheza tu abrakadabra za danganyatoto, ukweli wajulikana

JAMVI: ODM inacheza tu abrakadabra za danganyatoto, ukweli wajulikana

Na CHARLES WASONGA

SASA imedhihirika wazi kwamba kiongozi wa ODM Raila Odinga amejipata katika njiapanda kuhusu iwapo awanie urais 2022 au aunge mtu mwingine.

Hii ni kutokana na taarifa za kukanganya kutoka kwa chama hicho kuhusu suala zima la iwapo waziri huyu mkuu wa zamani ni miongoni mwa watakaoshindania tiketi ya ODM kuwania urais au la.

Wadadisi wanasema kuwa taarifa hizo kinzani kutoka kwa Bodi ya Kitaifa ya Uchaguzi (NEB) na afisi kuu ya chama hicho inaashiria kuwa Bw Odinga bado hajaamua iwapo atawania urais au aseme fulani “tosha”.

Siku moja baada ya mwenyekiti wa NEB Catherine Mumma kutoa taarifa iliyoorodhesha Bw Odinga miongoni mwa wale waliowasilisha maombi ya kutaka kuwania urais kwa tiketi ya ODM, Katibu Mkuu Edwin Sifuna alitoa taarifa kinzani.

Katika taarifa yake aliyoitoa Ijumaa na iliyoshangaza wengi, Bw Sifuna alifafanua kuwa kiongozi wa chama hicho hajawasilisha ombi la kutaka kugombea urais 2022.Bw Sifuna alisema kuwa taarifa ya awali iliyoeleza kuwa Bw Odinga aliwasilisha ombi lake kwa NEB ilikuwa ni mzaha wa Aprili 1.

Hii huwa ni siku ya wajinga ambapo watu hutoa taarifa za uwongo kisha kuweka ukweli baadaye. “Siasa ni suala la kuchukuliwa kwa uzito kila siku isipokuwa Aprili 1. Tuliamua kuadhimisha siku ya wajinga kupitia taarifa yetu jana (Aprili 1, tukifahamu fika kwamba wenzetu katika sekta ya habari watafahamu hilo lakini inaonekana kuwa walinoa,” akasema Bw Sifuna.

Alisema wale ambao wako kwenye kinyang’anyiro cha tiketi ya ODM ni Gavana Ali Hassan Joho (Mombasa) na mwenzake wa Kakamega Wycliffe Ambetsa Oparanya; akieleza kuwa Odinga atatoa msimamo wake baada ya kura ya maamuzi kuhusu Mswada wa BBI.

Bi Mumma alipoulizwa kuhusu madai ya Bw Sifuna kwamba Bw Odinga hakuwa ametuma maombi, alisema kuwa bodi yake ilichapisha majina ambayo ilipokea kutoka kwa sekritariati ya ODM.

“Sisi tulichapisha majina ambayo tulipokea kutoka wa sekritariati kuu ambako barua za maombi zilikuwa zikiwasilishwa. Ukitaka maelezo zaidi, tafadhali walisiliana na Katibu Mkuu au sekritariati,” Dkt Mumma akasema.Mchanganuzi wa masuala ya siasa Bw Mark Bichachi sasa anasema kuwa kuna uwezekano mkubwa kwamba taarifa ya Sifuna ilichochewa na mkutano kati ya Rais Uhuru Kenyatta na Bw Odinga.

“Mabadiliko haya yamechangiwa na hatua ya Uhuru kumpigia simu Raila kabla ya kumtembelea nyumbani kwake Karen. Hatua hii ilionekana kama ya kutuliza kambi ya kiongozi huyo wa ODM ambayo imekuwa ikilalamikia kile inachodai ni hujuma kutoka kwa Afisi ya Rais,” asema Bw Bichachi.

Kwa mujibu wa mdadisi huyo, taarifa iliyotolewa na NEB na iliyoorodhesha Mbw Odinga, Joho na Oparanya kama watu waliokuwa wamewasilisha maombi yao na stakabadhi husika kufikia tarehe ya mwisho, Machi 31, 2021, ilikuwa sahihi.

“Taarifa ya NEB ilikuwa sahihi kwa sababu ilitolewa baada ya Raila kuongoza mkutano wa Kamati Simamizi ya Kitaifa (NMC) nyumbani kwake Jumatano. Hii ni baada ya madaktari kuthibitisha kwamba alikuwa amepona corona,” asema Bichachi.

“Lakini baada ya kupata hakikisho kutoka kwa Rais Kenyatta kwamba mchakato wa BBI ungalipo, Raila aliamuru kwamba jina lake liondolewe kutoka kwenye orodha hiyo, kama hatua ya kimkakati,” anasema.

Kauli ya Bw Bichachi inashabihiana na yake wakili James Mwamu ambaye anaongeza kuwa Bw Odinga alikuwa anaelekea kugura handisheki na BBI hadi pale Rais Kenyatta alipoingilia kati.

“Uliposikia watu kama Orengo, Sifuna na wabunge Junet Mohamed na Otiende Amollo wakimshambulia Kibicho kwa kile walichodai ni kuhujumu ndoto ya Raila kuingia Ikulu ilikuwa dalili tosha kwamba uhusiano kati ya Uhuru na Raila ulikuwa umeanza kudorora. Hii ndiyo maana ilimlazimu Rais Kenyatta kumfikia Raila kusudi atulize hali,” anasema Bw Mwamu ambaye pia ni wakili.

“Bw Sifuna asidanganye kwamba taarifa ya NEB ilitolewa kimzaha kuadhimisha Siku ya Wajinga, Aprili 1. Ukweli ni kwamba aliagizwa kutoa taarifa aliyoitoa Ijumaa baada ya mashauriano ya Jumatano kati ya Rais na Raila,” asema mwenyekiti huyo wa zamani wa Chama cha Wanasheria Afrika Mashariki (EALS).

Itakumbukwa kwamba mwezi jana Bw Orengo (James) ambaye ni Seneta wa Siaya, Amollo (Mbunge wa Rarieda) na Mohamed (Mbunge wa Suna Mashariki) walimwelekezea kidole cha lawama Dkt Kibicho wakidai anamhujumu Bw Odinga kwa lengo la kuzima ndoto yake ya kuingia Ikulu 2022.

Aidha, walidai kuwa Katibu huyo ameteka mchakato wa BBI, kwa lengo la kumweka kando Bw Odinga.Hapo ndipo kuliibuka madai ya uwezekano wa kiongozi huyo wa ODM kushirikiana na Naibu Rais Dkt William 2022 na hivyo kusababisha wasiwasi katika kambi ya Rais Kenyatta.

Ni wakati huo ambapo mwenyekiti wa ODM John Mbadi na Mbunge wa Ugunja Opiyo Wandayi walionya kwamba huenda handisheki ikasambaratika ikiwa Rais Kenyatta hataingilia kati na kurekebisha hali.Hata hivyo, walisema kuwa Bw Odinga yu mbioni kubuni muungano mwingine wa kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2022.

Ilidaiwa kuwa washirika watarajiwa katika muungano huo ni; waziri wa zamani Mukhisa Kituyi, Gavana Kivutha Kibwana (Makueni) Charity Ngilu (Kitui) miongoni mwa wengine.

Hii ni baada ya fununu kutokea kwamba huenda Rais Kenyatta anaunga mkono muungano changa wa One Kenya Alliance unaoshirikisha waliokuwa vinara wenzake katika uliokuwa muungano wa upinzani (Nasa).

Wao ni Kalonzo Musyoka (Wiper), Musalia Mudavadi (ANC) na Moses Wetang’ula (Ford Kenya); na ambao wameshirikiana na mwenyekiti wa Kanu Gideon Moi.

Mbw Bichachi na Mwamu wanakubaliana kwamba, Bw Odinga atatoa mwelekeo kuhusu iwapo itawania urais au la kutegemea msimamo wa mwisho ambao Rais Kenyatta atatoa kuhusu suala hilo.

You can share this post!

One Kenya Alliance ina mchongoma wa kupanda kisiasa

JAMVI: Hivi anavyokuja Obado, ndiye kizibo cha Raila Nyanza?