• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:45 AM
KAULI YA MATUNDURA: Wataalamu wa Kiswahili wamuenzi galacha, mwalimu na mlezi wa wengi Prof Ireri Mbaabu

KAULI YA MATUNDURA: Wataalamu wa Kiswahili wamuenzi galacha, mwalimu na mlezi wa wengi Prof Ireri Mbaabu

Na BITUGI MATUNDURA

JUMA lililopita, hafla mbalimbali za kumuenzi na kumsherehekea mwalimu wa wengi – Prof George Ireri Mbaabu zilifikia kileleni kwa kongamano la webina lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Kenyatta.

Mkuu wa Idaya ya Kiswahili ya chuo hicho – Dkt Pamela Ngugi alisema, mbali na kuandaa dhifa ya kumshukuru na kumuaga Prof Mbaabu ambaye amefundisha Chuoni Kenyatta kwa zaidi ya miongo minne, Idara pia inadhamiria kuchapisha kitabu maalum kitakachowapa fursa wanataaluma wa Kiswahili kuandika makala kumhusu msomi huyo na mchango wake katika tasnia ya Kiswahili.

Mada ya webina hiyo iliyoandaliwa mnamo Machi 2, 2021 ilikuwa ni ‘Ukuzaji na Maendeleo ya Kiswahili’.

Wawasilishaji walikuwa ni pamoja na Prof Chacha Nyaigotti Chacha (Kamisheni ya Vyuo Vikuu, CUE-Kenya), Dkt Musa Hans (Naibu Mkurugenzi, TATAKI, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam), Maprof Sheila Ryanga, Kitula King’ei na Catherine Ndungo – wote wa Chuo Kikuu cha Kenyatta. Waratibu wa webina hiyo walikuwa ni Dkt Leonard Chacha Mwita, Bi Evelyne Mudhune, Dkt Pamela Ngugi na Dkt Richard Makhanu Wafula.

Akiifungua rasmi webina hiyo, Makamu Mkuu wa Chuo cha Kenyatta, Prof Paul K. Wainaina alimtaja Prof Mbaabu kuwa mwalimu, mshauri, mlezi na mwelekezi ambaye kwaye wanafunzi na wataalamu wengi walipitia mikononi mwake. Makamu Mkuu wa Chuo cha Kenyatta – Taaluma, Prof Paul Okemo alisema, “Wakati wako umefika kuondoka kwenye ulingo wa ‘kucheza densi’. Umekwisha kuwafundisha wacheza densi wa kutosha – na hata kama umeng’atuka, densi bado itaendelea katika kumbi za mihadhara kwa muda mrefu siku za mbeleni.”

Alimtaja Prof Mbaabu kuwa msomi mwenye nidhamu na bidii aliyetimiza malengo yake.

Prof Paul Wainaina alieleza kwa uketo safari ndefu ya Prof Mbaabu katika ulingo wa usomi. Prof Mbaabu alijiunga na Chuo Kikuu cha Nairobi mapema miaka ya 1970 – kusomea Kiswahili, Sosholojia na Elimu. Mnamo 1973, alikwenda katika Chuo Kikuu cha California, Los Angeles nchini Marekani kusomea shahada yake za uzamili (Masters) katika taaluma ya isimu.

Mnamo 1975, aliajiriwa na Chuo Kikuu cha Kenyatta alikofundisha kama Tutorial Fellow. Mnamo 1981, alikwezwa ngazi kuwa mhadhiri. Mnamo 1988, alikwenda katika Chuo Kikuu cha Howard – Washington DC kusomea shahada yake ya Uzamifu (PhD). Prof Mbaabu amewahi kuwa mshauri wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) mbali na kutuzwa na Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili (sasa Taasisi ya Taaluma za Kiswahili) mnamo 2005. Kwenye wasilisho lake, msomi na mhakiki, Prof Kitula King’ei alisema: “Prof Mbaabu ni mtu mwenye bidii na nidhamu kazini; mtenda haki aliyewasaidia wanafunzi wengi kupata nafasi za ufadhili wa masomo […] alinitia ari ya kuandika na kuchapisha jinsi alivyofanya yeye.”

Mchango wa Prof Mbaabu katika taaluma ya Kiswahili unaonekana bayana katika makala yake kwenye majarida ya kitaaluma barani Afrika, Asia, Marekani na Ulaya.

Baadhi ya vitabu vyake maarufu vinavyotumika kama marejeleo muhimu katika taasisi za elimu kote ulimwenguni ni pamoja na : Sheng –English Dictionary ; aliyoandika kwa ushirikiano na Nzuga Kibande (TUKI,2003), Historia ya Usanifishaji wa Kiswahili (TUKI,2007), New Horizons in Kiswahili : A Synthesis in Development Research & Literature (KLB,1978) na Language Policy in East Africa: A Dependency Theory Perspective (ERAP,1996). Riwaya yake ya hivi majuzi ni Masomoni California (Longhorn,2017)

[email protected]

You can share this post!

SAUTI YA MKEREKETWA: Viongozi Afrika hawana punje ya...

GWIJI WA WIKI: Franklin Mukembu