• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 6:50 AM
GWIJI WA WIKI: Franklin Mukembu

GWIJI WA WIKI: Franklin Mukembu

Na CHRIS ADUNGO

KUWA na mwelekeo chanya ni sifa ya lazima kwa binadamu yeyote yule mwenye maono endelevu kushikilia kikiki faulu ndipo afaulu kwa lolote lile analolifanya au analonuia kulitenda.

Yeyote anayelenga kufanikiwa maishani na kitaaluma sharuti atawaliwe na matumaini yasiyofifia ili aweze kuhimili panda-shuka za kila sampuli bila ya kupoteza mwelekeo ambao unadhibiti misingi ya malengo au maazimio yake.

Kama ilivyo katika biashara, kuna wakati wa kupata faida na vilevile kuna wakati wa kupata hasara. Hivyo ndivyo hali ilivyo hata kwa mwandishi. Kuna uwezekano wa kuiandika kazi bila ya kuchapishwa; lakini ukiwa na mwelekeo chanya, utaweza kuvumilia bila ya kukata tamaa wala kusita kuandika tena.

Jambo la muhimu katika kutenda lolote ulifanyalo ni kujiweka katika nafasi ya pili ili kuweza kushughulikia wengine kwanza. Hili litakuondolea ubinafsi na bila shaka matokeo yatawaridhisha wengine kisha utulivu na amani itasheheni katika moyo na nafsi yako.

Mhusika Amani katika riwaya yake Marehemu Ken Walibora ya ‘Kidagaa Kimemwozea’ anashikilia kuwa licha ya mswada wake kuibwa; cha maana mno ni kwamba hatimaye ulichapishwa na ujumbe aliotaka uwafikie wasomaji uliwafikia kwa njia iliyofaa.

Huu ndio ushauri wa Bw Franklin Mukembu – mwandishi chipukizi na mshairi shupavu ambaye kwa sasa ni mwalimu wa Kiswahili na somo la Jiografia katika Shule ya Upili ya Munithu, eneo la Imenti Kaskazini, Kaunti ya Meru.

MAISHA YA AWALI

Mukembu amewahi kuwaelekeza wengi wa wanafunzi wake kutunga mashairi ambayo yamewahi kuchapishwa katika gazeti la Taifa Leo.

Tangu 2016, Mukembu amekuwa mtahini wa Baraza la Kitaifa la Mitihani (KNEC). Yeye hushughulikia Karatasi ya Kwanza ya Kiswahili (Insha KAR 102/1). Tajriba anayojivunia katika utahini na usahihishaji wa karatasi hiyo imempa fursa ya kuzitembelea shule mbalimbali ndani na nje ya Kaunti za Meru na Tharaka-Nithi kwa nia ya kuhamasisha, kushauri na kuelekeza walimu na wanafunzi kuhusu njia na mbinu mwafaka zaidi za kujiandaa kwa mitihani ya kitaifa ya KCSE.

Mukembu amewashirikisha wengi wa wanafunzi wake katika mashindano ya mara kwa mara ya Digital Essay yanayoendeshwa na Shirika la eKitabu. Mnamo 2018, mwanafunzi wake aliambulia nafasi ya tatu na kujizolea zawadi ya rununu na kitita cha Sh10,000 katika Kitengo cha Uandishi wa Insha za Kiswahili yenye mada ‘Teknolojia Katika Kufanikisha Elimu kwa Wote’. Mnamo 2019, mwanafunzi wake aliibuka mshindi nambari tatu katika Kitengo cha Kiswahili kwa kuandika insha iliyohusu jinsi ya kutatua mahudhurio mabaya shuleni kwa kutumia teknolojia.

Makala yake ya kwanza kuchapishwa katika gazeti la Taifa Leo ni Barua kwa Mhariri ambapo aliwashauri wachambuzi wa magazeti katika vituo mbalimbali vya runinga na redio wachambue pia gazeti la Taifa Leo kama walivyokuwa wakifanya kwa machapisho mengine.

Kabla ya kufuzu kwa shahada ya kwanza, Mukembu alipata kazi ya muda ya kufundisha katika Shule ya Wavulana ya Kiriani, eneo la Maara, Kaunti ya Tharaka-Nithi.

Makala yake ya kwanza katika gazeti la Daily Nation yalichapishwa mnamo Novemba, 30, 2009 katika ukumbi wa ‘Letter to the Editor’ ambapo alieleza kuhusu umuhimu wa kuwatayarisha wanafunzi vyema na mapema ili kuzuia visa vya udanganyifu katika mitihani ya kitaifa.

TUZO

Mnamo 2010, Mukembu aliandika shairi la kumtumbuiza Mbunge wa Imenti Kaskazini, Kaunti ya Meru katika hafla ya kutoa zawadi kwa wanafunzi waliofaulu vyema katika mtihani wa kitaifa wa KCSE kutoka Shule ya Kutwa ya Munithu. Shairi hilo lililokaririwa na wanafunzi, lilimvunia Mukembu tuzo ya haiba na ya kutamanika mno.

Mnamo 2014, Mukembu alimtungia mwalimu wa shule moja ya msingi katika Kaunti ya Embu shairi ambalo liliwatambisha wanafunzi wake hadi kiwango cha kitaifa katika tamasha za muziki na drama. Shairi hilo lilikuwa lenye mada ‘Mitaa ya Mabanda’.

Mwaka wa 2018, alitunga shairi kuhusu Supa Bima (Bima ya Hospitali ya NHIF). Lilikaririwa na Kundi La wanafunzi 18 kutoka Shule ya Upili ya Munithu hadi kiwango cha kitaifa katika Chuo Kikuu Cha Dedan Kimathi mjini Nyeri.

Mukembu amewahi pia kutambuliwa na kutuzwa pakubwa na shirika lisilo la kiserikali la GEC ambalo liliwahi kudhamini hafla ya kutuzwa kwa wanafunzi waliong’aa katika mitihani na fani nyinginezo.

Mwaka uo huo, alimwongoza mwanafunzi wake kuandika insha ya kidijitali na akaibuka nambari ya tatu katika ushindi uliomvunia Mukembu cheti pamoja na vocha ya Sh1,000. Hafla ya kutolewa kwa tuzo hizo iliandaliwa katika Jengo la Sarit Centre, eneo la Westlands, Nairobi.

JIVUNIO

Zaidi ya kuwa mkereketwa wa lugha ya Kiswahili, Mukembu pia anajivunia natija si haba kutokana na uelekezi wa michezo ya kuigiza, utunzi wa michezo hiyo na uchoraji wa mandhari mbalimbali kwa minajili ya michezo ya drama (back drops).

Nyakati za tamasha za muziki na drama, Mukembu huandikia walimu wa shule za msingi na upili mashairi ya ngonjera, ya kukaririwa na vikundi vya wanafunzi au hata mwanafunzi mmoja kwa malipo ya kati ya Sh2,500 na Sh4,000. Mukembu pia ni mwamuzi stadi wa mashairi na maigizo katika mashindano ya shule, makanisa na mashirika mengine.

You can share this post!

KAULI YA MATUNDURA: Wataalamu wa Kiswahili wamuenzi...

NASAHA: Mwandalie mwanao jukwaa la kuyaratibu malengo yake...