• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 8:27 PM
18 wafariki kwenye ajali mbili tofauti Kisumu, Kilifi

18 wafariki kwenye ajali mbili tofauti Kisumu, Kilifi

CHARLES LWANGA na ALDRIN OCHIENG

WATU 18 walifariki Jumatano kwenye ajali mbili tofauti za magari katika kaunti za Kilifi na Kisumu.

Kwenye ajali ya Kilifi, watu 14 walifariki papo hapo na mmoja akipelekwa hospitalini, baada ya basi la Muhsin kugongana ana kwa ana na matatu eneo la Kwa Shume, barabara kuu ya Mombasa kuelekea Malindi.

Kamishna wa Kaunti ya Kilifi, Kutswa Olaka, aliyeongoza polisi na maafisa wa Msalaba Mwekundu kuokoa majeruhi, alisema madereva wote wawili walifariki dunia papo hapo.

“Ajali hii imehusisha basi ya Muhsin linalosimamiwa na Garissa Sacco, ambalo lilikuwa likisafiri kutoka Mombasa kuelekea Garissa na matatu ya Sabaki Travellers Shuttle iliyokuwa inatoka Malindi kuelekea Mombasa,” akasema. Bw Olaka.

Walioshuhudia walisema basi la Muhsin lilipoteza mwelekeo baada ya kupasuka gurudumu na kugongana na matatu hiyo.

Msimamizi wa hospitali kuu ya kaunti ndogo ya Malindi, Dkt Joab Gayo, alisema aliona miili 14 ambayo ilipelekwa katika chumba cha maiti.

“Tulipokea watu 18 wakiwa wamejeruhiwa. Kati yao sita waliokuwa katika hali mahututi wamepelekwa hospitali Mombasa kwa matibabu maalum,” akasema.

Dkt Gayo alisema watu wengine waliojeruhiwa kwenye ajali hiyo walipelekwa katika hospitali za kibinafsi kama vile Tawfiq na Star mjini Malindi.

Dereva wa basi la Simba Coach, ambaye alikuwa safarini wakati wa mkasa huo, alimlaumu mkandarasi anayepanua barabara kuu ya Malindi- Mombasa kwa kuchukua muda mrefu.

“Inawezekana mabonde na mashimo kwenye barabara hii inayoendelea kupanuliwa yamechangia kupasuka kwa gurudumu. Tunaomba serikali imhimize akamilishe kazi hii ambayo imechukua muda mrefu,” akasema dereva huyo.

Kamishna wa Kaunti ya Kisumu, Samuel Anampiu kwa upande wake alisema lori la kubeba miwa liliacha njia likiwa kwenye kivuko kwenye barabara ya juu ya Kachok eneo la Nyamasaria na kuanguka umbali wa mita 20.

“Dereva wa trela hilo la kubeba miwa alikufa papo hapo. Watu wawili aliokuwa nao walikufa walipokuwa wakikimbizwa hospitalini,” alisema Bw Anampiu.

Magari mawili yaliyokuwa yakioshwa chini ya barabara hiyo ya daraja yaliharibiwa.

Hata hivyo, hayakuwa na watu wakati wa ajali hiyo.

Trela hilo lilikuwa likisafirisha miwa kutoka eneo la Awasi.

Kulingana na Bernard Otieno, ambaye alishuhudia ajali hiyo, trela lilikuwa likipanda kwa kasi mno. Vijana ambao huosha magari chini ya mwinuko huo wa barabara walikimbilia usalama wao.

Miili ya waliokufa ilipelekwa katika chumba cha maiti ch hospitali ya Mafunzo na Rufaa ya Jaramogi Oginga Odinga.

You can share this post!

Hasira za raia zashtua serikali

Shirika laonya kuhusu nyama