• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
UHURUTO WALIVYOFUTA REKODI YA KIBAKI

UHURUTO WALIVYOFUTA REKODI YA KIBAKI

BENSON MATHEKA NA PAUL WAFULA

MATATIZO ya kiuchumi yanayokumba Kenya kwa wakati huu yanatokana na hatua ya serikali ya Jubilee kudunisha demokrasia na sera za kiuchumi ambazo ambayo Wakenya walifurahia katika utawala wa miaka 10 wa Rais Mstaafu Mwai Kibaki, wataalamu wanasema.

“Demokrasia ndiyo oksijeni inayofanya uchumi kukua na maendeleo kupatikana. Unapoua demokrasia na kuzima uhuru wa raia kujieleza huwa unaua uchumi wa nchi,” asema Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Kimataifa kuhusu Sera na Migogoro, Ndung’u Wainaina.

Alipokabidhi madaraka kwa Rais Uhuru Kenyatta na William Ruto mnamo Aprili 9, 2013, Mzee Kibaki aliwaambia kuwa amewaachia nchi iliyokuwa tayari kupaa kiuchumi na ustawi.

Lakini miaka tisa baadaye ndege ya uchumi iko katika hali mbaya zaidi, na itachukua juhudi kubwa kuirudisha katika hali aliyoiacha Mzee Kibaki.

Mara baada ya kupokea madaraka, utawala wa Jubilee ulipuuza sera za kiuchumi za Mzee Kibaki zilizosaidia Kenya kustawi kiuchumi bila ukopaji.

Rais Kenyatta na Dkt Ruto walianza utekelezaji wa miradi mikubwa mikubwa waliyofadhili kwa mikopo.

Hii ndiyo sababu deni la Kenya limepanda kutoka Sh1.8 trilioni aliloacha Mzee Kibaki hadi Sh7.2 trilioni kufikia mwishoni mwa mwaka jana.

Madhara ya deni hili ni uchumi hafifu huku serikali ikianza kuchelewesha mishahara ya wafanyikazi wake na pesa za kaunti.

Mzee Kibaki alipostaafu, kila Mkenya alikuwa akidaiwa Sh40,000, lakini sasa kila mwananchi anadaiwa Sh137,000.

Hali pia ni mbaya hivi kwamba kwa kila Sh100 zinazokusanywa na KRA kama ushuru, Sh60 zinatumiwa kulipa madeni.

Hii imelazimisha serikali kuendelea kuwaongezea Wakenya ushuru licha ya matatizo yanayowakabili kutokana na kuzorota kwa uchumi na janga la Covid-19.

Utawala wa Mzee Kibaki ulifanikiwa kupunguza kutegemea mikopo na kuondoa Kenya chini ya minyororo ya mashirika ya IMF na Benki ya Dunia.

Bw Wainaina anasema kilichosaidia zaidi utawala wa Mzee Kibaki kujenga uchumi imara ni kudhamini demokrasia na utawala wa sheria.

Anasema chini ya utawala wake, Mzee Kibaki aliruhusu Wakenya kukosoa serikali na kutumia maoni yao kuimarisha uchumi wa nchi bila kuwatisha.

“Kibaki alikumbatia maoni ya kufaa nchi ya wakosoaji wake wakuu. Hakujibizana nao au kutumia idara za usalama kuwanyamazisha. Watu waliomtusi walitembea huru bila wasiwasi wa kukamatwa. Pia aliruhusu bunge kutekeleza majukumu yake kwa njia huru tofauti na inachofanya serikali ya Jubilee,” asema Bw Wainaina.

Mzee Kibaki pia aliruhusu upinzani ndani ya serikali yake na alichotarajia kutoka kwa maafisa wake ni utendakazi.

Kulingana na Bw Wainaina, uchumi wa nchi hauwezi kustawi iwapo serikali inapuuza utawala wa sheria ambao ni nguzo ya demokrasia.

“Wawekezaji huwa wanakosa imani na nchi ambayo serikali haiheshimu utawala wa sheria na kukiuka maagizo ya mahakama,” asema kuhusu hulka ya Rais Kenyatta na maafisa wakuu wa serikali yake kudharau maagizo ya mahakama. Kulingana na Bw Wainaina, Jubilee imewafunga vinywa Wakenya na kuwatisha ili wasiulize maswali wanapokadamizwa.

“Kibaki aliamini kuwa serikali ni ya raia na sio walio mamlakani. Aliruhusu upinzani kuendelea kukosoa serikali na kwa kufanya hivi aliweza kujua maafisa waliokuwa wakizembea kazini na hivyo kumwezesha kuchukua hatua. Hakuwa na kisasi na upinzani au waliomkosoa kwa kuwa aliheshimu demokrasia,” asema mwanaharakati Lucia Ayiela wa Kongamano la Mageuzi. Wanaharakati wanasema serikali inayoua demokrasia hufanya hivyo kwa nia ya ku maovu na udhaifu wake.

“Wanataka kuwatoza Wakenya ushuru, wakope na watumie pesa kwa njia isiyoeleweka lakini wasiulizwe maswali. Wakati wa Kibaki, Wakenya walifichua kashfa bila hofu yoyote ya kukamatwa,” asema.

Muungano wa Mashirika ya Kutetea Haki za Binadamu unasema kushuka kwa demokrasia nchini kulishika kasi 2018.

Watetezi hao wanasema ni wazi kuwa Kenya imerejea katika enzi za utawala wa mabavu, ambao ulitumbukiza Kenya katika hali mbaya ya kiuchumi miaka ya themanini na tisini. Kwa upande wake serikali inasema kwamba haki zote zina mipaka, na Wakenya hawafai kutumia uhuru wanaohakikishiwa na Katiba kukiuka sheria wakisingizia demokrasia.

You can share this post!

Siku mbili zatenganisha kifo cha mwanamuziki Albert Gacheru...

Kenya sasa yaanza kujitengenezea silaha