• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 9:35 PM
Kenya yaomba mkopo mwingine wa Sh86 bilioni kutoka Benki ya Dunia

Kenya yaomba mkopo mwingine wa Sh86 bilioni kutoka Benki ya Dunia

Na CHARLES WASONGA

LICHA ya pingamizi kutoka kwa Wakenya, serikali inaendelea na mtindo wake wa kuomba mikopo kutoka kwa taasisi za kimataifa kufadhili mahitaji yake wakati huu wa janga la corona.

Hazina ya Kitaifa inasema inaendelea na mazungumzo na Benki ya Dunia (WB) kwa nia ya kupata mkopo mwingine wa Sh86 bilioni, siku mbili baada ya Wakenya kulalamikia mkopo wa Sh255 bilioni kutoka kwa Shirika la Fedha Ulimwenguni (IMF).

Kwenye taarifa, Waziri wa Fedha Ukur Yatani alisema mkopo huo ambao utatolewa chini ya kitengo cha maendeleo katika benki hiyo, yaani Word Bank Development Policy Operations (DPO).

“Mazungumzo yanaendelea baada ya Kenya kuwasilisha ombi lake katika bodi ya wakurugenzi wa Benki ya Dunia ndani ya majuma kadha yajayo. Ikiwa mazungumzo hayo yatafaulu, tutapokea mkopo huo Mei au Juni 2021,” Yatani akasema Jumatano baada ya kufanya mazungumzo na Taufila Nyamadzabo, ambaye ni mkurugenzi mkuu wa benki hiyo, kanda ya Afrika.

Mnamo Mei 2020 Kenya ilipokea mkopo wa Sh106 bilioni kutoka Benki ya Dunia kuisaidia kufadhili bajeti yake na kukinga uchumi kutokana na athari zilizosababishwa na janga la Covid-19.

Mkopo huo utalipwa kwa kipindi cha miaka 30.

Kenya imeomba mkopo mwingine kutoka Benki ya Dunia siku chache baada ya IMF kuidhinisha mkopo wa Sh255 bilioni hatua ambayo ilichochea pingamizi nyingi kutoka kwa Wakenya katika mitandao ya kijamii.

Wakenya hao waliilaumu serikali ya Rais Uhuru Kenyatta kwa kuwawekea mzigo mkubwa wa madeni ambao sasa imefika Sh8 trilioni kuanzia mwezi wa Januari.

Hata hivyo, waziri Yatani amepuuzilia mbali pingamizi hizo akishikilia kuwa Kenya ina uwezo wa kumudu mikopo yake na itatumia pesa hizo kwa njia nzuri.

Aliahidi kutoa maelezo ya kina kuhusu mikopo hiyo hivi karibuni ili kuzuia “Wakenya kupotoshwa na watu fulani ambao lengo lao kuu ni kuichafulia serikali jina.”

You can share this post!

KASHESHE: Sioni tena nikiwahi kuwa mke wa mtu!

Hazina ya Kitaifa yalaumiwa kwa uzorotaji wa huduma vituo...