• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 1:51 PM
Supamaketi zina kibarua kudhibiti msongamano wa watu kipindi hiki cha janga la Covid-19

Supamaketi zina kibarua kudhibiti msongamano wa watu kipindi hiki cha janga la Covid-19

Na SAMMY WAWERU

LICHA ya serikali kuhimiza maeneo yanayotoa huduma za umma yadhibiti kiwango cha watu wanaoingia mara moja, maduka ya kijumla yangali na kibarua kigumu.

Kufuatia uchunguzi wa Taifa Leo katika supamaketi kadhaa mitaa mbalimbali Nairobi na Kiambu, misongamano ya wateja inaendelea kushuhudiwa kwenye foleni ya kashia.

Mfano, katika maduka ya kijumla ya Kassmatt Jumbo na Naivas eneo la Githurai, msongamano wa watu umekuwa si hoja kwa wahudumu na wasimamizi.

Taswira hiyo si tofauti na ya duka la jumla la PowerStar mtaa wa Zimmerman, kati ya mengine, hali hiyo ikiweka wafanyakazi na wateja wenyewe katika hatari ya kuambukizwa virusi vya corona.

“Ndio tunaelewa ni hatari, ila wateja nao hawatilii maanani maelekezo tunayowapa. Ni Mungu tu anatulinda,” akasema mhudumu mmoja wa duka la Naivas.

Msongamano huo wa wanunuzi unaibua maswali chungu nzima, kuhusu usalama wa taifa, maduka tuliyozuru yakiashiria taswira ya mengine.

Maji yanazidi unga kuanzia mwendo wa adhuhuri, kizungumkuti ambacho kinazua wasiwasi, ikizingatiwa kuwa hakuna anayejua hali ya mwenzake iwapo ameambukizwa virusi au la.

Licha ya maelekezo na ilani kuwekwa katika maduka hayo, wateja wameendelea kupuuza, na ni jukumu la wahudumu kuwakumbusha.

Kiambu na Nairobi ni miongoni mwa kaunti ambazo zimetajwa kuwa hatari katika maambukizi ya corona.

Rais Uhuru Kenyatta alitangaza Machi 26, 2021, kukaza kamba kanuni na mikakati zilizowekwa kusaidia kuzuia corona, katika kaunti hizo mbili pamoja na Kajiado, Machakos na Nakuru.

Kenya inaendelea kuandikisha ongezeko la maambukizi, ikiwa ni pamoja idadi ya wanaoangamizwa na Covid-19.

Ni muhimu maduka ya jumla nchini yachukue tahadhari ya hatari inayowakodolea macho.

Hatua ya Rais Kenyatta kutangaza kusimamisha kwa muda mikutano ya umma, na inayoandiliwa kudhibitiwa idadi ya watu, maduka ya kijumla yanapaswa kuiga mkondo huo.

You can share this post!

Hazina ya Kitaifa yalaumiwa kwa uzorotaji wa huduma vituo...

Visa vya wizi wa ng’ombe vyazidi Gatundu Kaskazini