• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 1:51 PM
TANZIA: Mume wa Malkia Elizabeth II wa Uingereza afariki

TANZIA: Mume wa Malkia Elizabeth II wa Uingereza afariki

MASHIRIKA na SAMMY WAWERU

MUME wa Malkia Elizabeth II wa Uingereza, Prince Philip ameaga dunia Ijumaa akiwa na umri wa miaka 99.

Tangazo hilo limetolewa na Kasri la Buckingham.

“Ni kwa masikitiko makubwa Malkia ametangaza kifo cha mume wake, Prince Philip,” inaeleza taarifa hiyo iliyochapishwa katika akaunti ya Twitter ya Kasri hilo.

Ikaongeza taarifa: “Alifariki kwa amani asubuhi ya leo (Ijumaa), Windsor Castle. Matangazo zaidi yatatolewa baadaye,” Kasri la Buckingham limesema.

Waziri Mkuu wa Uingereza, Boris Johnson ametuma salamu zake za pole kwa familia ya Malkia Elizabeth II, akisema amepokea habari hizo kwa mshangao na huzuni.

“Alikuwa mshirika wa kifalme aliyehudumu kwa muda mrefu. Ni mmoja wa walioshiriki Vita vya Pili vya Dunia na alitajwa kuwa Shujaa. Prince Philip alisaidia kuongoza familia ya Kifalme na Ufalme ili iweze kuwa taasisi muhimu,” akasema Waziri Mkuu Boris.

Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta katika risala zake za rambirambi amemfariji Malkia Elizabeth II, Familia ya Kifalme, Waziri Mkuu Boris Johnson na raia wa Uingereza.

Rais Kenyatta amesema Philip amekuwa nguzo ya umoja ulimwenguni.

“Mstahiki Prince Philip amekuwa ishara kuu ya maadili ya familia na umoja wa raia wa Uingereza na vile vile jamii ya kimataifa. Hakika, tunamwomboleza mtu mashuhuri aliyependa utangamano wa amani miongoni mwa wanadamu,” amesema Rais Kenyatta.

Akiwa mume wa Malkia Elizabeth II, alimsaidia kuongoza kwa kipindi cha muda wa miaka 65 mfululizo, hadi kustaafu kwake 2017.

Amekuwa nguzo kuu kwa Malkia kwa zaidi ya miaka 70. Cheo chake kimekuwa ni ‘Duke wa Edinburgh’.

Mwendazake ametajwa kusaidia kuboresha miradi mbalimbali ya maendeleo Uingereza.

Aidha, alikuwa mtoto wa kipekee wa kiume wa Mwanamfalme Andrew wa Ugiriki na Mwanamalkia Alice wa Battenberg.

Pamoja na Malkia Elizabeth II, walikuwa wamejaliwa kupata watoto wanne, wajukuu wanane na vitukuu 10.

You can share this post!

Mwanabodaboda apigwa faini ya Sh11,000

Waliopatikana na pombe kituo cha polisi wachekesha korti