• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 5:23 PM
Ubakaji: Mahakama yanyima 2 dhamana

Ubakaji: Mahakama yanyima 2 dhamana

Na RICHARD MUNGUTI

MWANAFUNZI wa Chuo Kikuu aliyeshtakiwa pamoja na mwanamume anayedaiwa huwabaka wasichana wa vyuo vikuu, wamenyimwa dhamana na mahakama ya Kibera, Nairobi.

Hakimu Mwandamizi, Bi Esther Boke alisema Faith Washiali Bwibo na Abdirizak Adan Abdullahi ni hatari kwa usalama wa walalamishi, na itabidi wazuiliwe gerezani hadi kesi isikizwe na kuamuliwa.

Bi Boke alikubaliana na kiongozi wa mashtaka Bw Allan Mogere kuwa Abdirizak, anayemiliki bastola atavuruga haki kwa kutoa vitisho kwa mashahidi wanaotazamiwa kufika kortini kuelezea kufafanua madai yao.

Hakimu alisema washtakiwa hao wawili watapewa fursa siku za usoni kuwasilisha upya ombi lao la kuachiliwa kwa dhamana “baada ya mashahidi wakuu kufika kortini kuelezea kilichojiri.”

“Hii mahakama haiwezi kufunga macho na masikio isisikie kilio cha walalamishi ambao wameelezea hofu kwamba wametishwa na kupata kichapo cha nguruwe walipokataa kuitikia matakwa ya mshtakiwa (Abdirizak),” alisema hakimu.

Bi Boke pia alisema alimsikiza baba ya mmoja wa walalamishi ambaye ni wakili mwenye tajriba ya juu aliposema “naumwa sana na kitendo hiki cha mshtakiwa wa kwanza kumbaka binti yangu na kumtupa jangwani aliwe na fisi. Mshtakiwa huyu hana utu hata!”

Hakimu alisema upande wa mashtaka umewasilisha ushahidi wa kutosha kwamba washtakiwa watavuruga haki na “hata kuwatishia maisha walalamishi.”

Akasema, “Ili haki ionekane ikitendeka basi washtakiwa hawa watasalia gerezani hadi upande wa mashtaka uwasilishe ushahidi.”

Hakimu aliamuru kesi itajwe tena Aprili 20, 2021.

Hakimu alielezwa kuwa Abdirizak anaishi katika mtaa wa maafisa wakuu wa Jeshi (KDF).

Korti ilielezwa ni vigumu walalamishi na polisi kuingia mtaani humo kwa vile uko chini ya ulinzi mkali masaa 24.

Mahakama ilielezwa Abdrizak, “yuko na ashiki ya hali ya juu na hamu iliyopitiliza na kuthubutu kuwapepeta wasichana huku amewashikia bastola vichwani.”

Bw Mogere alipinga vikali mshukiwa huyo kuachiliwa kwa dhamana akisema “ni hatari kwa usalama wa kitaifa na pia kwa wasichana wa vyuo vikuu na wale walio balehe.”

Korti pia iliombwa imzuilie mshtakiwa huyo kwa hofu ya kuwachafua wasichana wenghine waliopo likizoni baada ya shule kufungwa.

Wakati huo huo, Bw Mogere alisema ingawa mshtakiwa anamiliki bastola polisi bado hawajafanikiwa kuipata.

“Abdullahi huyu hana utu. Alimbaka mteja wangu katika mtaa wa Mugoya ulioko eneo la South C kaunti ya Nairobi. Pia akimtumia Faith Washiali Bwibo, alimsaliti na kumpeleka mlalamishi tena eneo duni kaunti ndogo ya Naivasha, ambapo alimtupa kwenye jangwa usiku aliwe na wanyama mwitu baada ya kukataa dhuluma zake za kimapenzi.” wakili anayemwakilisha mwathiriwa, Bi Amazon Koech alieleza mahakama.

You can share this post!

Wawili wazuiliwa kwa mauaji

Mumewe Malkia wa Uingereza aaga dunia