• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:40 AM
FUNGUKA: ‘Usinihukumu; napenda kuvalia mavazi ya kike’

FUNGUKA: ‘Usinihukumu; napenda kuvalia mavazi ya kike’

Na PAULINE ONGAJI

KATIKA ulimwengu huu uliojaa vituko kila kuchao, hata katika masuala ya mahaba, maajabu hayakosi.

Na hakuna anayewakilisha taswira hiyo vyema kama Phillip. Kwanza kabisa Phillip ni mwanamume wa mika wa 37 mkazi wa eneo la Nairobi.

Kwa zaidi ya mwongo mmoja sasa amekuwa akifanya kazi kama msimamizi wa mojawapo ya mashirika makubwa ya kimataifa hapa nchini.

Bwana huyu ameweza kujiundia himaya ya mali katika sehemu mbali mbali nchini. Kutoka kwa majumba ya kifahari, hadi kwa magari ya uchukuzi, na fleti za nyumba za kukodesha, ni dhahiri kwamba kaka huyu kifedha amejihami vilivyo.

Tukija katika masuala ya kimaumbile, ni madume wachache ambao wanaweza jisimamisha kwenye orodha sawa na kaka huyu.

Utanashati wake ni wa kustaajabisha. Dume limeumbwa likaumbika. Vituguta vyake ni thabiti kana kwamba Maulana alipomuumba alitumia patasi yenye ncha kali kuchonga sehemu hii kwa ukamilifu.

Kwenye mashavu yake kamilifu kuna vibonyo vinavyobonyea ndani kila anaposema au kucheka, na kuonyesha meno yake yaliyojipanga kinywaani kwa laini nyoofu.

Umbo lake pia ni la kipekee. Mbali na kimo chake cha kati, kifua chake kipana na thabiti, kinahitimisha baadhi ya sifa zinazomfanya kuwa kivutio cha mabinti wengi.

Lakini licha ya sifa hizi zote, kaka huyu amekuwa na changamoto ya kupata mpenzi, mchumba au mke wa kudumu, kutokana na sababu anazofahamu mwenyewe:

“Napenda kuvalia suruali na mavazi mengine ya ndani ya wanawake ninapolala. Kwa hivyo ninapolala lazima nivalie chupi, sidiria na kamisi.

Na sio kwamba navalia mavazi mapya, la! Lazima yawe yale ambayo mpenzi au mchumbangu amevalia na hayajasafishwa. Namaanisha kwamba ikiwa umevalia mavazi haya mchana kutwa, ukija na kuyatoa nyumbani, usiyasafishe, bali unipe nami niyavalie usiku kucha.

Kuna wale wanaoshindwa kuelewa naridhika vipi tu kwa kufanya hivyo? Jibu ni sahili, kuyavalia tu, kunashibisha njaa yangu ya mahaba.

Kumbuka kwamba kwangu hayo ni mahaba tosha. Nikiyavalia tu sina haja ya kumgusa au kushiriki mahaba na binti yeyote.

Kwa hivyo ukitaka kuwa mchumba wangu basi ujiandae kunihudumia kwa kunipa mavazi yako ya ndani tu! Ngoma sina haja nayo, kwa maana kuwa hata watoto sitaki.

Lakini mimi sio mchoyo. Ukiwa mpenzi au mchumba wangu na kukubali masharti yangu, niko tayari kukuruhusu kuwa na uhusiano wa pembeni mradi tu ukirejea nyumbani, nami utanihudumia kwa njia hiyo.

Ni jambo ambalo limeninyima fursa ya kuwa na mchumba au mke wa kudumu. Wengi ninaokutana nao wanavutiwa na uzuri vile vile utajiri wangu, lakini inapowadia wakati wa kushibisha kiu yangu ya mahaba kuambatana na mbinu yangu, wengi hutoweka.

Kuna wale ambao mwanzoni hujaribu kuvumilia, lakini muda unavyozidi kusonga wanashika njia na kutoweka.

Lakini licha ya haya, sina nia ya kulegeza msimamo wangu na kamwe sitamlazimisha yeyote kukaa nami. Ikiwa unataka kuwa nami njoo, lakini sahau mahaba na mapenzi mengine ya kawaida. Mahitaji yako ya kifedha yatakidhiwa vilivyo lakini upande huo mwingine, sahau.”

You can share this post!

Viongozi wamuomboleza mume wa Malkia Elizabeth

Bunge halitachelewesha BBI – Muturi