• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 6:55 AM
KAMAU: Wajibu wa serikali kuhakikishia wanahabari usalama

KAMAU: Wajibu wa serikali kuhakikishia wanahabari usalama

Na WANDERI KAMAU

MNAMO Aprili 10, 2020, dunia nzima iliamkia habari za kusikitisha kuhusu kifo cha msomi na mwanahabari maarufu, Prof Ken Walibora.

Prof Walibora alikuwa ametoweka kwa siku kadhaa, ndipo shughuli za kumtafuta alikokuwa zikaanza.

Juhudi za kubaini kitendawili hicho ziliishia katika mochari ya Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta (KNH), ambako mwili wake ulipatikana.

Licha ya kuenziwa na wengi kwa mchango mkubwa aliotoa katika ukuzaji wa lugha ya Kiswahili na mawanda mengine ya kiusomi, kifo cha Prof Walibora kimebaki fumbo hadi sasa.

Hakuna aliyekamatwa wala kufunguliwa mashtaka, licha ya ahadi ya serikali kusaka na kuadhibu waliohusika kwenye mauaji hayo ya kikatili.

Inasikitisha kuwa wakati maadhimisho ya mwaka mmoja tangu kifo cha Prof Walibora yanaendelea, tasnia ya uanahabari nchini inaomboleza tena mauaji ya kikatili ya mwanahabari mwingine.

Bi Betty Barasa, aliyehudumu kama mhariri wa video katika shirika la habari la KBC, aliuawa kikatili na watu wasiojulikana nyumbani kwake katika eneo la Ngong, Kaunti ya Kajiado, Jumatano usiku wakati akirejea nyumbani kutoka kazini.

Kulingana na taarifa za polisi, marehemu aliuawa na watu hao baada yao kukosa pesa walizokuwa wakitafuta nyumbani kwake.

Kama kawaida, Idara ya Kuchunguza Uhalifu (DCI) imeahidi kufanya kila iwezalo kuhakikisha waliohusika kwenye ukatili huo wamebainika na kuchukuliwa hatua za kisheria.

Mauaji ya Bi Barasa yanatokea wiki mbili tu baada ya mauaji ya mwanahabari mwenzake, Bi Jennifer Wambua, aliyehudumu kama afisa wa mawasiliano katika makao makuu ya Wizara ya Ardhi, jijini Nairobi.

Bi Wambua alipatikana ameuawa kikatili katika msitu wa Ngong, Kajiado, baada ya kutoweka kwa siku kadhaa.

Bila shaka, hivi ni visa vinavyoonyesha kuwa maisha ya wanahabari si salama hata kidogo nchini.

Maisha yao yamegeuka kuwa ya roho mkononi. Wanaishi kwa hofu na mashaka kwamba, huenda wakaandamwa na mahasimu wao kutokana na majukumu wanayotekeleza katika jamii.

Maswali yanaibuka: Ni lini serikali itawahakikishia usalama wanahabari?

Tangu 2013, serikali ya Jubilee imekuwa ikiingilia uhuru wa wanahabari kiasi cha kufananisha majukumu yao na “uenezaji porojo tu.”

Katika nchi zilizostawi kidemokrasia, vyombo vya habari ni miongoni mwa taasisi zinazoheshimika sana na jamii. Katiba ya Kenya i wazi pia kuhusu haki za wanahabari.

Wanahabari si maadui wa raia. Si maadui wa nchi. Ni wazalendo wanaopaswa kulindwa kwa kila hali.

[email protected]

You can share this post!

Mumewe Malkia wa Uingereza aaga dunia

MUTUA: Napongeza na kushabikia Tanzania chini ya Suluhu