• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
MUTUA: Napongeza na kushabikia Tanzania chini ya Suluhu

MUTUA: Napongeza na kushabikia Tanzania chini ya Suluhu

Na DOUGLAS MUTUA

MMOJA kati ya Wakenya waliomshabikia sana marehemu rais wa Tanzania, John Magufuli, ni mwanahabari mwenzangu aliyedai Rais Samia Suluhu Hassan, atafuata nyayo za mtangulizi wake.

Alitumia uteuzi wa Makamu wa Rais, Dkt Philip Mpango, kama ushahidi kwamba genge la Magufuli lingali linashika usukani wa nchi.

Si kweli! Mambo yamebadilika tayari. Vyombo vya habari vilivyokandamizwa na kufungiwa na Magufuli viko huru sasa, sikwambii hata Corona inashughulikiwa kisayansi!

Tanzania ya Magufuli ilionekana kufuata nyayo za Ethiopia, enzi ya marehemu waziri mkuu Meles Zenawi, aliyevinyanyasa vyombo vya habari.

Labda Rais Hassan amesikia kilio cha kiongozi wa upinzani, Bw Tundu Lissu, aliyewahi kunukuliwa akieleza jinsi uchumi wa Tanzania ulivyokua enzi ya Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete kutokana na uhuru wa kujieleza na kuchangamana.

Mswahili husema mtenda kazi asishe ni sawa na asiyetenda; Bi Hassan anapaswa kuwaachia huru kikamilifu wanahabari na Watanzania kwa ujumla.

Hili ni muhimu hasa ikizingatiwa Rais mwenyewe aliviagiza vyombo vilivyofungiwa vifuate sheria za nchi.

Je, vitazifuataje sheria vilizodaiwa kuvunja kabla ya kufungiwa bila kujibana kiusemi au kujiachia na kuhatarisha kufungiwa tena?

Pa kuanzia ni Rais kuagiza vipengee kandamizi viondolewe kabisa kwenye sheria za nchi ili asije nduli mwingine kama Magufuli asizuke kavitumia kuirejesha nchi Misri.

Watanzania wana jukumu la kutekeleza katika upatikanaji wa uhuru wa wanahabari na wa kujieleza.

Wanapaswa kuishinikiza serikali ifanye mabadiliko ili matamanio yao yawekwe kwenye sheria za nchi, wasiketi kitako na kuamini serikali itawafanyia hisani.

Wanafaa kujua serikali hiyo tu iliyowapa uhuru inaweza kuutwaa kwani hakuna sheria zinazoizuia kufanya hivyo.

Uhusiano kati ya watawala wa nchi na vyombo vya habari tangu hapo ni wa kimapambano, mmoja asipepese jicho kwani serikali haina hulka ya kutenda hisani.

Kila wakati serikali inapotaka kufanya mambo yasiyofaa, wahanga wa kwanza ni wanahabari kwa kuwa wako chonjo daima na hawasiti kufichua maovu yakitokea.

Hata Bi Hassan mwenyewe akitaka kufanya kitu, mfano kutunga sera zisizo maarufu, watu wa kwanza kunyamazisha watakuwa wanahabari. Hisani yake ni ya muda.

Kwamba Rais huyo ana ukakamavu wa kukubali ushauri wa kisayansi kuhusu jinsi ya kukabiliana na Corona ni ithibati ya kujitenga na u-Magufuli.

Kuwaongoza Watanzania kuachana na gangaganga za mitishamba alizosifia si haba marehemu Magufuli ni hatua ya kijasiri inayoweza tu kuchukuliwa na anayejiamini.

Dunia inatazama na inapendezwa na uamuzi huo; hivi karibuni utasikia mataifa tajiri yakitua Tanzania na misaada ya chanjo na dawa. Hili litawezekana kwa urahisi kwa kuwa Waziri wa Mambo ya Nje, Bi Liberata Mulamula, ameagizwa airejeshee Tanzania mahusiano mema.

Kama Mkenya, natarajia Bi Mulamula aimarishe uhusiano kati ya Kenya na Tanzania ili nikienda zangu Dar es Salaam na Zanzibar nisihisi kama nalazimisha undugu.

[email protected]

You can share this post!

KAMAU: Wajibu wa serikali kuhakikishia wanahabari usalama

TAHARIRI: Chanjo inatolewa sasa michezo irudi