• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 7:50 AM
TAHARIRI: Chanjo inatolewa sasa michezo irudi

TAHARIRI: Chanjo inatolewa sasa michezo irudi

KITENGO CHA UHARIRI

HATIMAYE, zoezi la kuchanja wanasoka nchini dhidi ya virusi vya corona linang’oa nanga rasmi hii leo katika uwanja wa Kasarani, kukiwa na matumaini tele kwamba mechi za kandanda zitarejelewa tena hivi karibuni.

Takriban dozi 700 zitatolewa kwa wachezaji na maafisa wa klabu mbalimbali za Ligi Kuu ya Kenya (KPL) kwanza, kabla baadaye kupewa wanasoka wa timu za wanawake, Ligi ya Kitaifa ya Supa (NSL) na ligi za chini.

Zoezi la leo linafuatia lile la kuwachanja wanamichezo wa timu za taifa zitakazowakilisha Kenya katika michezo ya Olimpiki na mingine ya kimataifa mwaka huu, lililoanza Alhamisi.

Katika shughuli hii wizara za Michezo na Afya zinalenga watu 3,500 katika timu hizo; kuanzia wanamichezo, makocha, maafisa wa michezo na mtu yeyote yule anayehusika moja kwa moja na wanamichezo kote nchini.

Zoezi hili la utoaji chanjo pia limeshuhudia maafisa wa mbio za magari za Safari Rally wakipokea dozi hiyo muhimu, wanapojiandaa kwa mashindano ya kimataifa baadaye mwezi Juni.

Rais Uhuru Kenyatta alipositisha tena michezo kufuatia wimbi la tatu la corona, aliweka kipaumbele utoaji chanjo kama kigezo muhimu katika kuondoa marufuku hiyo. Hii ikitekelezwa sambamba na masharti yale mengine ya kuvaa maski wakati wote ukiwa nje katika maeneo ya umma, kunawa mikono kwa maji na sabuni au kutumia sanitaiza, na kuepuka mikusanyiko.

Pilkapilka hizi zote za utoaji chanjo ni habari njema, na dhihirisho la jinsi wizara na mashirikisho ya michezo zinajitahidi kuhakikisha uhondo wa mechi na mashindano unarejelea tena viwanjani.

Fani ya michezo ni sekta muhimu sana nchini. Kando na uhondo huo kwa maelfu ya mashabiki, kunao watu wengi tu wanaoenda viwanjani kwa madhumuni ya kufanya mazoezi ya mwili.

Kubwa zaidi, sekta hii ni kitega uchumi kwa maelfu ya watu walioajiriwa humo moja kwa moja au wanahusika kwa njia nyingine. Ujira huu wote umekwama kwa sasa sababu ya corona huku maelfu ya wanamichezo wakikosa la kufanya nyumbani.

Hivyo, tunasihi wizara za michezo na afya pamoja na mashirikisho yote ya michezo kuvalia njuga suala hili la chanjo ili kuhakikisha wanamichezo, maafisa na kila mhusika anapokea kinga hii muhimu.

You can share this post!

MUTUA: Napongeza na kushabikia Tanzania chini ya Suluhu

FATAKI: Ajabu jamii kutilia shaka werevu wa binti kwa...