• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 6:55 PM
MWANAMUME KAMILI: Usijitie zuzu, tia bidii kujua yanayomhusu mke wako

MWANAMUME KAMILI: Usijitie zuzu, tia bidii kujua yanayomhusu mke wako

Na DKT CHARLES OBENE

MNAOJITUMA kufa kupona wenzenu kuwapa nafsi na moyo vilevile, sikateni tamaa wala kushika tama na kusononeka kwa tabia za wafidhuli wanaume wa leo.

Baadhi ya wanaume wa leo wanafanya dharau kwa kutojua tu. Ipo siku wanaume majefule watakuja tambua utamu wa mapera msimu wa maembe ujapo kwisha. Hakuna haja ya michirizi ya chozi wala kamba shingoni kufia mahabani!

Kutojua jambo sio ujinga; ujinga ni kukataa kujifunza! Kuna baadhi ya wanaume wenye akili za nanga hata kujifunza ni kazi. Uzito huu wa akili unatokana na tabia za wanaume wa leo kutopenda kujuzwa ya hekima. Wanajifanya kujua kila kitu. Hawaambiliki hawasemezeki!

Hakuna azaliwaye mjuvi wa mambo na vijimambo duniani. Hakuna msomi kwa mambo ya nyumbani ama chumbani. Sote ni wanafunzi tunaopata funzo moja baadha ya nyingine kila kukicha. Wanaume kwa wanawake wamejanjarukia mengi kuyajulia ukubwani. Aidha kutokana na kuelimishwa, kujuzwa, kunong’onezewa ama kuuliza tu hasa akina sisi tusiojua kuficha fundo moyoni. Hivyo basi sina shaka kwamba mwanamume kutojua jambo ni mwenyewe kupenda. Isitoshe, mwanamume kukataa kuelimika ni kwa raha zake.

Kuna mengi ambayo wanaume wa leo wameyafumbia macho na kujifanya hawajui! Kweli sijaelewa jinsi mwanamume anavyoweza kupachika mimba na mwishowe kukataa kuwajibikia malezi ya mwanawe akitilia shaka asili na fasili ya mtoto yule. Vipi mtu kutilia shaka uzao wa mtoto katika dunia hii ya teknohama?

Huwa wapi hawa wanaume wanaoibuka na kuwakana watoto wakijua wazi walifanya mambo ya wakubwa? Ama ndio nyie mnaojua kupanda ila kuvuna. Ndio wao hao wanaopanda kitandani na madaftari ama majadala kuyasoma wakati watu wazima wanakuwa shughulini.

Ndio wao hao wanaopokea simu na kujadili biashara kwa lisali moja tena usiku wa manane wakiwa juu ya mnara. Ndio wao hao wanaokesha mitandaoni ya kijamii ilhali wanawajibikia shughuli za watu wazima.

Jamani zindukeni nyie wenye kuwafanyia wenzenu dhihaka kama hizo!

Inachukiza mwisho wa chuki mtu kukufanyia dharau sampuli ile. Mwenzio kajisabilia kwako mwili na nafsi, fikra na akili, pumzi na uhai wala huoni haja kumpa hata tone la heshima? Madaftari na majalada ya kusomwa usiku wa manane ndio heshima? Ndio heshima anayostahili mke kwa kukuchagua wewe na kukufanya mtu mbele ya watu? Nyie wanaume wa leo mna nini? Afadhali mwenye kukupa talaka kuliko mwanamume apandaye kitandani na rununu na kujadili biashara wakati mkewe anasubiri kupanda wanakopanda waliojazibika kimahaba! Afadhali mtu kusalia peke yake maishani kama mwezi kuliko kudunishwa namna ile.

Heri kuzama baharini na kuliwa na samaki kuliko dharau sampuli ile. Komeni nyie wanaume wenye maudhi na dharau hizi! Nani kawaambia wanawake hawana biashara ama hamu ya kusoma majalada na madaftari kitandani? Hebu kivalie kiatu cha mwenzio kabla kumdunisha namna ile. Tabia hizi hazina nafasi katika meza ya watu wanaothamini wenzao.

Tulivyo wachapa kazi, baadhi yetu tunasingizia shughuli aina ainati kama sababu ya kupitwa na mengi ya chumbani na vilevile nyumbani. Ukweli ni kwamba baadhi yetu ni wanaume limbukeni tusiopenda kujituma kimaisha na kujua mambo yanayohusu mke. Ndio maana wanaume wa leo hawachelei kukana watoto kama kwamba hawakuhusika walivyohimilika mama yao.

La ajabu ni kwamba hata kuuliza siku za hedhi tunaona kama kazi ya sulubu. Ndio maana wanawake wanalalama mno kwenye nyumba na vyumba vya watu wazima! Afadhali hata beberu maana anazo akili za kutoa ishara za kamba kukatikia malishoni! Mambo ya kuelimishana polepole kitandani ndio hayo tunayatolea macho.

Ukali wa baadhi ya wanaume wa leo unatokana hasa na akili zao butu. Kuna mambo ya chumbani wasiojua kaka zetu ila hawataki kuuliza! Mwanamume kamili ni akili. Misuli tuipeleke shambani au ukulini! Tatizo ni kwamba ni kwamba mwanamume wa leo anaona haya hata kumweleza mpenzi au mkewe kwamba hana pesa! Wachache mno wanaweza kukiri kwamba hali si hali mfukoni.

You can share this post!

Atwoli apewa miaka mingine mitano kutetea wafanyakazi

UMBEA: Hakuna mpenzi mzuri au mbaya inategemea tu ikiwa...