• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 3:25 PM
Mipango kuandaa Muturi kuwania urais 2022 yaiva

Mipango kuandaa Muturi kuwania urais 2022 yaiva

Na ALEX NJERU

YAMKINI juhudi zinaendelea za kuandaa Spika wa Bunge la Kitaifa Justin Muturi kuwa kigogo wa siasa za eneo la Mlima Kenya na hata kuwania Urais baadaye mwaka 2022.

Kutawazwa kwa Bw Muturi kama msemaji wa jamii za Mlima Kenya na wazee wa Kiama Kiama (Kikuyu), Nyangi Ndiririri (Embu), Ngome (Mbeere) na Njuri Ncheke (Meru na Tharaka) sasa kunamweka kama mwanasiasa mwenye mamlaka zaidi eneo la Mlima Kenya baada ya Rais Uhuru Kenyatta.

Ingawa mwanzoni kutawazwa kwake kuliibua nyufa za kisiasa mlimani, baadhi ya wanasiasa waliokuwa wakimpinga awali sasa wamerejea katika kambi yake huku mikakati ya kisiasa ikiendelea kupangwa kuhakikisha anadhibiti eneo hilo kisiasa.

Japo Rais Kenyatta hajawahi kuzungumzia hadharani kutawazwa kwa Bw Muturi, wandani wake sasa wanamuunga mkono mbunge huyo wa zamani wa Siakago na hata kudai kwamba yeye ndiye kiongozi ambaye anapendelewa na Rais.

Baadhi ya wanasiasa nao wamekuwa wakimtembelea nyumbani kwake Kanyambora kimya kimya huku madiwani wa Tharaka Nithi wakawa kati ya wanasiasa ambao wameonyesha uaminifu wao kwa Spika Muturi.

Mnamo Alhamisi, madiwani hao wakiongozwa na Spika David Mbaya na Kiongozi wa wengi Peterson Mwirigi walimtembelea Bw Muturi nyumbani kwake na kumpa mbuzi wawili wakubwa ishara kuwa wanakubali uongozi wake.

Bw Mwirigi alisema kiongozi wa hadhi eneo hilo baada ya Rais Kenyatta eneo la Mlima Kenya, Bw Muturi anafaa kwa wadhifa wa urais kwa kuwa alihudumu kama mbunge kwa mihula miwili na pia spika kwa muda huo.

Kiongozi wa wachache Wilson Nyaga naye alisema ni wakati wa kiongozi kutoka Mlima Kenya Mashariki kutoa kiongozi mpya wa eneo hilo. Kaunti za Tharaka-Nithi, Embu na Meru ndizo zinapatikana Mlima Kenya Mashariki.

“Kwa zaidi ya miaka 60 uongozi wa eneo hili umetokea Magharibi mwa mlima huu na sasa ni wakati wa kiongozi kutokea Mlima Kenya Mashariki,” akasema Bw Nyaga.

Diwani maalum Millicent Mugana naye amewataka wakazi wote wa kaunti za Mlima Kenya wamuunge mkono Bw Muturi ili ashinde kiti cha Urais 2022.

Baadhi ya madiwani wa kaunti ya Tharaka-Nithi ambao walikuwa wakimuunga mkono Naibu Rais Dkt William Ruto nao wamevuka na sasa wapo mrengo wa Bw Muturi.

Katika kaunti nzima ya Tharaka Nithi, ni Seneta Kithure Kindiki amesalia kambi ya Dkt Ruto.

Taifa Leo imebaini kwamba, madiwani kutoka Kaunti ya Meru wanapanga kumtembelea Bw Muturi nyumbani kwake kueleza uaminifu wao na kumpigia upato 2022.

Bw Muturi mwenyewe amewashukuru madiwani hao kwa kuonyesha imani katika uongozi wake na akawataka wahakikishe wanawahudumia raia vyema na waungane pamoja ili kuzungumze kwa sauti moja katika siasa za kitaifa.

“Tumakinikie umoja wetu na kuwahudumia vyema waliotuchagua,” akasema Bw Muturi.

Kando na wanasiasa, Bw Muturi amekuwa akishauriana na viongozi wa kijamii, wale wa dini na wafanyabiashara ili kujitafutia umaarufu.

You can share this post!

Mikopo: Wakenya wamchangia mwanaharakati

CHOCHEO: Kukataa mchezo wa huba ni kuhatarisha ndoa –...