• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 8:12 PM
CHOCHEO: Kukataa mchezo wa huba ni kuhatarisha ndoa – Washauri

CHOCHEO: Kukataa mchezo wa huba ni kuhatarisha ndoa – Washauri

Na BENSON MATHEKA

CIDY anajuta kumkaushia mumewe Zack kwa uroda alipokataa kumnunulia zawadi siku yake ya kuzaliwa.

Zack alivumilia kwa miezi miwili akitumia kila mbinu kumshawishi Cidy lakini akakataa kumtimizia haki yake ya tendo la ndoa kisha akaamua kutafuta huduma kwingine na kumpata Rose ambaye baada ya kuchepuka naye mara tatu, alimweleza alikuwa na mimba yake.

“Uhusiano wangu na Zack umeingia doa na sasa anataka kumuoa Rose. Makosa yalikuwa yangu. Kama singemnyima haki yake ya tendo la ndoa singekuwa katika hali hii,” asema Cidy.

Ndoa yao ni ya kitamaduni na kisheria, Zack anaruhusiwa kuoa zaidi ya mke mmoja. Katika kisa sawa na cha Cidy, Kimani anasema kwamba mkewe alichepuka na mpenzi wake wa zamani baada ya kukosa kumchangamkia kitandani kwa miezi minne.

“Tulikosana nilipogundua kwamba alikuwa amechukua mkopo na kununua nyumba bila kunifahamisha. Japo sio vibaya kufanya hivyo, tuligombana na nikahama chumba cha kulala licha yake kutumia kila mbinu nirudi ikiwa ni pamoja na kuniomba msamaha na kunikabidhi stakabadhi zote za nyumba aliyonunua. Baadaye niligundua alikuwa akimchangamkia mpenzi wake wa zamani na nikajuta kwa tabia yangu,” asema Kimani.

Ingawa mkewe aliungama kwamba hakuwa amezini na jamaa huyo, Kimani alihisi kwamba tabia yake ilihatarisha ndoa yake na akatafuta ushauri nasaha kutoka kwa wataalamu ambao waliwapatanisha.

Kulingana na Dick Ipetu, mshauri mwandamizi katika shirika la Abundant Love jijini Nairobi, wachumba huwa wanaweka uhusiano wao kwenye hatari wanapokaushiana uroda baada ya kutofautiana na kugombana.

“Ni kweli ugomvi huwa unavuruga uhusiano kati ya wanandoa lakini wanaponyimana haki ya tendo huwa wanaangamiza ndoa yao. Ni kawaida ya tofauti kuzuka na kufanya mtu kukosa hisia za mapenzi kwa mwenzake lakini ili kuokoa ndoa, suluhu inafaa kupatikana haraka kabla ya jahazi kuzama,” aeleza Ipetu. Hivi ndivyo Cidy alikosa kufanya na ndoa yake sasa iko mashakani.

Wataalamu wa masuala ya ndoa wanasema kwamba haki ya tendo la ndoa ni gundi inayounganisha wachumba na mtu hafai kumnyima mwenzake kumwadhibu wanapotofautiana.

“Inasukuma mtu kuwa na mipango ya kando na huu ndio ukweli na ikifikia hapo huwa kuna uwezekano wa kuvunjika kwa ndoa na kusababisha majuto,” asema Ipetu.

Kulingana na Pasta Winnie Kibui wa shirika la First Love Restoration Center jijini Nairobi, kunyima mchumba wako haki ya tendo la ndoa bila sababu maalumu ni sawa na kujiondoa katika ndoa.

“Wakati ambao wanandoa hawafai kushiriki tendo la ndoa ni mmoja wao akiwa mgonjwa. Kuna wanandoa wanaoishi miji tofauti na kwa sababu wanajua siri hii wanasafiri muda mrefu kuhakikisha kuwa wanapeana haki yao ya ndoa. Ajabu ni kwamba unapata wanaoishi nyumba moja wananyimana kwa sababu ya mambo madogo wanayoweza kuepuka au kusuhuhisha,” asema Kibui.

Kulingana na wataalamu, wachumba wanaponyimana tendo la ndoa huwa wanatumbukiza wenzao kwa majaribu.

“Kwanza, unamtumbukiza mtu kwenye mateso ya kisaikolojia na kumweka katika majaribio. Akipata mtu wa kumchangamkia atapita naye na utakuwa umevuruga uhusiano wako,” asema.

Kulingana na Pasta Kibui, watu wakioana huwa ni kitu kimoja na kinachowaunganisha ni tendo la ndoa.

“Kama hakuna sababu ya kimazingira au maradhi, sioni sababu ya mtu kumnyima mpenzi wake haki ya ndoa. Ni sawa na kunyima mwili wako kwa kuwa mtu na mkewe ni kitu kimoja,” asema.

Hata hivyo, asema ili kufurahia tendo lazima kuwe na uhusiano mwema kati ya wachumba.

“Epukeni mizozo, eleweni kuwa ni kawaida kuwa na tofauti za kimaoni ambazo kamwe, narudia, kamwe, hazifai kufanya mtu amnyime mwenzake haki yake ya ndoa na ikizuka hali ambayo hamchangamkiani, tafuteni ushauri kutoka kwa wataalamu na viongozi wa kiroho,” asema.

Kulingana na sheria ya ndoa ya Kenya, moja ya sababu za kuvunjika kwa ndoa ni kunyimana haki ya ndoa.

You can share this post!

Mipango kuandaa Muturi kuwania urais 2022 yaiva

Shujaa, Lionesses kurejea nyumbani leo Jumamosi kutoka raga...