• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 4:28 PM
Shujaa, Lionesses kurejea nyumbani leo Jumamosi kutoka raga ya Dubai

Shujaa, Lionesses kurejea nyumbani leo Jumamosi kutoka raga ya Dubai

Na GEOFFREY ANENE

TIMU za taifa za raga ya wachezaji saba kila upande za Kenya maarufu kama Shujaa (wanaume) na Lionesses (wanawake) zinatarajiwa kurejea nyumbani Aprili 10 baada ya kukamilisha raga ya Emirates Invitational 7s mjini Dubai, Ijumaa.

Shujaa ya kocha Innocent ‘Namcos’ Simiyu ilipepeta majirani Uganda 36-5 na kukamata nafasi ya tano kutoka orodha ya mataifa manane yaliwania taji la wanaume.

Lionesses ya kocha Felix Oloo ilimaliza ya mwisho baada ya kuoshwa 43-0 na Japan katika mechi ya kuamua nambari tano na sita (mwisho).

Mashindano haya yalitanguliwa na mazoezi ya siku nne. Shujaa ilikamilisha mashindano ya kwanza ya Dubai yaliyoandaliwa Aprili 2-3 katika nafasi ya tatu nayo Lionesses ilivuta mkia.

Vijana wa Simiyu walianza mashindano ya pili ya Dubai kwa kuzaba Uganda 28-10, Canada 21-10 na Uhispania 17-14 katika mechi za Kundi Buluu mnamo Aprili 8.

Mambo yaliwaendea vibaya katika mchuano wao wa kwanza wa siku ya pili walipolimwa 15-12 na Chile katika robo-fainali.

“Inasikitisha jinsi tulivyocheza dhidi ya Chile kwa kufanya makosa madogomadogo na mengine yasiyofaa ambayo mwishowe tuliishia kujuta kwa sababu tuliteremka hadi shindano la Sahani,” alisema Simiyu.

Vijana wake walijinyanyua katika nusu-fainali ya Sahani dhidi ya Uhispania.

“Tuliweza kufanya vitu kadhaa sawa ilivyotakikana dhidi ya Uhispania vilivyotusaidia kuwakanyaga 27-15. Tutaendelea kujiimarisha kwa sababu tunatumia mashindano haya kujipima kwa ajili ya Raga za Dunia na Michezo ya Olimpiki baadaye mwaka huu,” nahodha Andrew Amonde aliongeza.

Katika fainali ya Sahani, Jacob Ojee, Alvin Otieno na Vincent Onyala walipachika mguso mmoja kila mmoja naye Johnstone Olindi akafunga miguso miwili. Tatu kati ya miguso hiyo sita iliandamana na mikwaju. Uganda, ambayo inanolewa na Mkenya Tolbert Onyango, ilipata mguso mmoja kupitia kwa Aaron Ofoywroth.

Lionesses ilipata mafunzo kadhaa ya kutia moyo. Oloo na nahodha Philadelphia Olando walipongeza wachezaji kwa kuimarika.

Mabingwa hao wa Afrika mwaka 2018 walionyesha kuimarika dhidi ya wazoefu wa Raga za Dunia Canada na Amerika walipopoteza 22-5 na 22-10, mtawalia.

“Tulisumbua miamba hao. Unapolinganisha ukubwa wa vichapo tulipokea mwezi Februari mjini Madrid na hivi vya Dubai utaona tumepiga hatua. Bado kuna kazi kubwa ya kufanywa, hasa tunavyoanzisha mipira. Tuko asilimia 60 na tunahitaji kuwa juu zaidi ya hapo kabla tuende shindano la Los Angeles mwezi June,” alisema Oloo.

Nahodha msaidizi Sheila Chajira aliumia Alhamisi na kushauriwa apumzike siku kadhaa kabla ya kurejea uwanjani. Matokeo yote ya Lionesses ya Dubai: Aprili 8 – Canada 22 Lionesses 5, Ufaransa 31 Lionesses 5, Japan 10 Lionesses 10; Aprili 9 – Lionesses 12 Brazil 15, Amerika 22 Lionesses 10, Japan 43 Lionesses 0.

You can share this post!

CHOCHEO: Kukataa mchezo wa huba ni kuhatarisha ndoa –...

Karakara ni matunda ya thamani na rahisi kuyastawisha