• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 5:46 PM
Mwanajeshi aliyeshtakiwa kwa kosa la kudhulumu mtu aachiliwa huru

Mwanajeshi aliyeshtakiwa kwa kosa la kudhulumu mtu aachiliwa huru

Na BRIAN OCHARO

MWANAJESHI wa zamani, Swabir Abdulrazaq Mohamed, Ijumaa alipata afueni baada ya kupewa dhamana ya Sh50,000 kutokana na shtaka la kumpiga mtu na kumsababishia majeraha ya mwili.

Bw Mohamed, ambaye hadi Jumatatu alikuwa akifanya kazi Mombasa, alikanusha shtaka la kumshambulia Evans Odhiambo alipofikishwa mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Vincent Adet.

Upande wa mashtaka unadai mtuhumiwa pamoja na watu wengine ambao hawakuwa mahakamani, walifanya kosa hilo mnamo Septemba 14, 2020, katika eneo la Shimanzi, Mombasa.

Bw Mohamed alipewa dhamana licha ya pingamizi kutoka kwa Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma, ambayo ilitaka azuiliwe hadi mwathiriwa awekwe chini ya Mpango wa Kulinda Mashahidi.

“Mhasiriwa hana makazi na tunaogopa kwamba mshukiwa anaweza kumshawishi kabla ya kutoa ushahidi,” akasema kiongozi wa Mashtaka Ogega Bosibori. Pia Bi Bosibori aliambia korti kuwa umma bado una machungu na mshukiwa na kwamba kuzuiliwa kwake kutamhakikisha usalama wake.

“Hii pia ni kwa usalama wake mwenyewe kwa sababu tunahisi umma umemtambua vyema, na kwa hivyo itakuwa hatari kwake kuwa huru kuanzia sasa,” akaongeza.

Aidha Bi Bosibori alisema jambo hilo limevutia umma na kwa hivyo linapaswa kushughulikiwa kwa uangalifu mwingi. Bi Bosibori pia alidai kwamba wachunguzi bado hawajapata ushahidi katika eneo ambako mwanajeshi huyo alidaiwa kutenda kosa hilo.

Mawakili wa mshukiwa, Said Ali na Nabil Mohamed walipuuza madai ya upande wa mashtaka kuwa hayana msingi na kuhimiza korti impe dhamana. “Mshukiwa nii afisa wa zamani, ni raia anayetii sheria. Tunasihi korti isitilie maanani uvumi unaenzwa na upande wa mashtaka,” akasema Bw Ali.

Kwenye uamuzi wake, hakimu alikubaliana na mawakili hao na kusema kuwa upande wa mashtaka ulipaswa kutoa sababu zaidi zenye mashiko kuishawishi mahakama imzuilie mshukiwa.

Ombi kama hilo la kutaka mshukiwa azuiliwe kwa siku 14 zaidi lilikataliwa Jumatano huku mahakama ikiwapa wachunguzi siku tatu ya kukamilisha upelelezi wao. Upande wa mashtaka ulitaka wiki mbili ili kuwezesha maafisa wake kukagua kanda ya video kumtafuta mwathiriwa na pia kupata rekodi zake za matibabu.

Pia, ilitaka siku zaidi kuthibitisha ikiwa mwaathiriwa aliiba chochote, na ikiwa wizi huo ulirekodiwa katika kituo chochote cha polisi.

  • Tags

You can share this post!

Raila apewa ujumbe wa Ruto

Nahodha wa Changamwe Ladies aomba wadhamini wazisaidie...