• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 2:07 PM
ICC yadai Gicheru alihonga mashahidi wajiondoe kwa kesi

ICC yadai Gicheru alihonga mashahidi wajiondoe kwa kesi

Na WALTER MENYA

KESI inayomkabili wakili Paul Gicheru katika Mahakama ya Kimataifa kuhusu Uhalifu (ICC), imezingirwa na madai ya mashahidi kushawishiwa kuondoa ushahidi wao baada ya kupokea hongo.

Upande wa mashtaka ukiongozwa na Fatou Bensouda, unadai kwamba Bw Gicheru alitumia afisi yake katika jumba la Veecam, mjini Eldoret kukutana na mashahidi kisha kuwalipa ili wakatae kutoa ushahidi na pia kuondoa ule walikuwa wameuwasilisha kortini.

Stakabadhi kutoka ICC zilionyesha kwamba mashahidi hao walilipwa pesa taslimu ili kufuta ushahidi huo na wengi wao waliweka pesa zao kwenye benki. Baadhi walilipwa ili kuwashawishi wenzao waondoe ushahidi waliokuwa wamewasilisha ICC.

Kwa mujibu wa stakabadhi iliyochapishwa mnamo Ijumaa kutoka kortini, upande wa mashtaka ulieleza kwamba Bw Gicheru alikutana na mashahidi katika miji ya Eldoret, Nakuru, Nairobi na mingine kuwashawishi waondoe ushahidi wao.

Kwenye hati ya kukamatwa kwa mwanaharakati Walter Barasa ambaye alikuwa akidaiwa alihitilafiana na mashahidi, upande wa mashtaka unadai kwamba alisafiri hadi nchi jirani kuwahonga mashahidi ambao walikuwa wamepewa ulinzi.

“Gicheru alihusika pakubwa katika kuvuruga ushahidi na pia kuwashawishi mashahidi ambao walikuwa wakipewa ulinzi kwa kuwahonga. Hii ndiyo maana mashahidi wengi walijiondoa baada ya kupewa pesa hizo baadhi hata wakitishiwa maisha iwapo wangeghairi nia,” akasema Bi Bensouda katika kesi dhidi ya Bw Gicheru.

Mawakili wa Bw Gicheru tayari walisema kortini kwamba hawatawasilisha orodha ya ushahidi kwa kuwa Bi Bensouda ana kibarua kigumu cha kuthibitisha madai yote.

“Hatutawasilisha ushahidi wowote ila tunatarajia upande wa mashtaka uwasilishe ushahidi wake kisha wauthibitishe. Sheria za ICC zinakubali hili na tunasubiri pia kutetea mteja wetu,” akasema wakili wa Bw Gicheru, Bw Michael G Kamavaz wakati wa kikao kortini Aprili 8.

Hata hivyo, upande wa mashtaka unataka upande wa utetezi uwasilishe orodha ya ushahidi wake badala ya kutegemea wao.

“Ingawa kutoa ushahidi si lazima kwa mujibu wa sheria, kuwasilisha orodha ya ushahidi ni lazima,” akasema Bi Bensouda.

Wakati huo huo, mashahidi wanane ambao walikiri kuhongwa na Bw Gicheru walifichua mahakamani kuwa walilipwa mamilioni ya fedha ili waondoe ushahidi wao. Hata hivyo, walirejea kutoa ushahidi wao katika kesi hiyo ili kutafuta ulinzi baada ya kutishiwa maisha.

Upande wa mashtaka pia ulifichua kwamba ingawa mashahidi hao waliahidiwa mamilioni ya fedha, baadhi yao hawakulipwa pesa hizo zote na walipolalamika walitishiwa maisha.

Kwa mfano shahidi aliyesajiliwa kama P-0397 aliahidiwa Sh5 milioni iwapo angejiondoa kwenye kesi hiyo lakini akapokea Sh1 milioni pekee. Ingawa alikimbilia usalama wake na kupewa hifadhi na upande wa mashtaka, alitekwa nyara na akakosa kutoa ushahidi katika kesi dhidi ya Naibu Rais Dkt William Ruto na mwanahabari Joshua Arap Sang.

Shahidi mwengine aliyesajiliwa P-800 alidai kuwa aliahidiwa Sh2 milioni lakini akapokea Sh500,000 pekee kutoka kwa Bw Gicheru ili amshawishi shahidi mwengine ajiondoe katika kesi hiyo.

You can share this post!

Wahudumu 4,000 kupoteza kazi hoteli Pwani

Raila awindwa na Uhuru, Ruto