• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 8:55 AM
DINI: Dunia hii ina mitihani mingi, usitamauke, mtafute Mungu ndiye mtetezi wako

DINI: Dunia hii ina mitihani mingi, usitamauke, mtafute Mungu ndiye mtetezi wako

 

Na WYCLIFFE OTIENO

UMEWAHI kujipata katika hali ya mtihani mgumu?

Siku moja nilipata habari kumhusu mtu mmoja katika kijiji fulani nchini Congo. Bwana huyo alialikwa katika sherehe na alielekea kule kwa gari lake.

Akiwa njiani alifika pahali akashindwa kulidhibiti gari hilo likagonga mti uliokuwa kando ya barabara na kubingirika bondeni.

Lakini alibahatika kushika tawi la mti na akajipata amening’inia. Akamlilia Mungu sana amuokoe. Baada ya muda mrefu, akiwa hoi na amefikia mahali pa kukata tamaa, alisikia sauti ya Mungu.

Lakini alipuuza maana sauti ilimtaka afanye jambo la kipuuzi. Mara ya pili akasikia sauti ikisema, “Achilia!” Lakini akapuuza. Mara ya tatu akasikia sauti, “Kama waniamini achilia tawi hilo nikuokoe!” Alikemea sauti hiyo na akakataa kuachilia.

Huo ulikuwa mtihani mgumu sana. Lakini kuishi au kufa kwa huyu bwana kulitegemea kuiamini sauti ya Mungu na kutii. Wakati mwingi Mungu anatutarajia kufanya mambo ambayo ni magumu. Lakini huwa ameficha mafanikio yetu katika mambo hayo. Kama kweli tunamsadiki Bwana tutatii na kufanikiwa sana.

Maisha tunayoishi yamejaa mitihani migumu. Lakini Mungu ametupa uwezo wa kufanikiwa katika kila hali.

Wakati huu wa janga la corona, ni wakati mgumu. Hakika huu ni mtihani mgumu. Lakini Mungu ametupa uwezo wa kushinda. Mtihani huu pia utapita. Mungu hujitwalia utukufu katika mafanikio yetu. Tunachohitaji ni kumwamini na kumtumainia hata mtihani uwe mgumu kiasi gani.

Katika Mwanzo 22, Ibrahimu alijipata katika mtihani mgumu sana. Baada ya kupitia miaka mingi ya maudhi kwa kukosa mototo, Mungu akamkumbuka na kumbariki na Isaka. Alipokuwa anafikiria ni wakati wa kusherehekea, “Mungu alimjaribu Ibrahimu, akamwambia, Ee Ibrahimu! Naye akasema, Mimi hapa. Akasema, Umchukue mwanao, mwana wako wa pekee, umpendaye, Isaka, ukaende zako mpaka nchi ya Moria, ukamtoe sadaka ya kuteketezwa huko juu ya mlima mmojawapo nitakaokuambia.”

Lakini Ibrahimu akamtii Mungu na kuondoka ili aende kumtoa mwanawe kama sadaka ya kuteketeza. Ibrahimu alimsadiki Mungu. Ibrahimu alimtumainia Mungu. Ibrahimu alimwamini Mungu. Huu ulikuwa mtihani mgumu. Lakini hakuwa na shaka na Mungu. Alikumbuka alipokuwa miaka 75 Mungu alimtoa kwao na akaahidi kumbariki. Alipotimiza miaka 100 Mungu tayari alikuwa amedhihirisha uaminifu wake. Alijua kuwa aliyembariki mara ya kwanza, anaweza kumbariki mara ya pili

Ibrahimu alikuwa mtu wa imani. Ibrahimu alikuwa rafiki wa Mungu. Ukiwa na imani utakuwa rafiki wa Mungu. Mazingira yako yanaweza kuwa magumu, lakini imani yako inaweza kubadilisha matokeo.

Mchungaji John Maxwell alisema, “unaweza kukosa uwezo wa kubadilisha mazingira yako, lakini una uwezo wa kubadilisha mtazamo wako”.

Ibrahimu aliondoka akiwa na mtazamo chanya, licha ya mtihani mgumu. Mwanzo 22:4-5, “Siku ya tatu Ibrahimu akainua macho yake, akapaona mahali pakali mbali. Ibrahimu akawaambia vijana wake, Kaeni ninyi hapa pamoja na punda, na mimi na kijana tutakwenda kule, tukaabudu, na kuwarudia tena.”

Angalia Mtazamo wa Ibrahimu aliwaambia wajakazi wanaenda kuabudu halafu watarudi. Lakini kulingana na agizo la Mungu, Isaka hangerudi maana alienda kuteketezwa. Hata alipoulizwa na Isaka kuhusu sadaka, angalia alivyojibu. Mwanzo 22:6-8 “Basi Ibrahimu akazitwaa kuni za hiyo sadaka, akamtwika Isaka mwanawe; akatwaa moto na kisu mkononi mwake, wakaenda wote wawili pamoja.

Isaka akasema na Ibrahimu baba yake, akinena, Babangu! Naye akasema, Mimi hapa, mwanangu. Akasema, Tazama! Moto upo, na kuni zipo, lakini yuko wapi mwana-kondoo kwa sadaka ya kuteketezwa? Ibrahimu akasema, Mungu atajipatia mwana-kondoo kwa hiyo sadaka, mwanangu. Basi wakaendelea wote wawili pamoja.

Moyoni mwa Ibrahimu, alijua vyema kuwa anaenda kumtoa mwanawe kama sadaka ya kuteketeza. Lakini alimtumainia Mungu na alikuwa tayari kumtii katika kila hali. Hatimaye Mungu alijidhihirisha kwa kujitolea kondoo. Akapaita mahali pale Yehova-yire.

Usiogope unapojipata katika mtihani mgumu. Mungu atajitolea. Mungu atakutetea. Utafanikiwa katika mtihani huo. Hakuna jambo gumu kwa Mungu. Mtumainie, msadiki, mtegemee katika kila hali.

Vyote ulimwenguni na mbinguni ni mali yake. Palipohitajika damu ya mwanakondoo asiye na mawaa ili ulimwengu usamehewe, Mungu alimtoa mwanawe wa pekee Yesu Kristo. Tukimwamini tunapata uzima wa milele. Bwana atajitolea!

You can share this post!

MALENGA WA WIKI: Walibora aendelea kukumbukwa kwa mchango...

Rais aomboleza kifo cha mamake aliyekuwa Katibu wa Wizara...