• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 10:55 AM
Rais aomboleza kifo cha mamake aliyekuwa Katibu wa Wizara El-Maawy

Rais aomboleza kifo cha mamake aliyekuwa Katibu wa Wizara El-Maawy

CHARLES WASONGA na PSCU

RAIS Uhuru Kenyatta ametuma risala za rambirambi kwa familia, jamaa na marafiki wa Mama Shariffa El-Maawy ambaye alifariki Jumapili nyumbani kwake Nairobi akiwa na umri wa miaka 89.

Mama Shariffa ni mamake aliyekuwa Katibu katika Wizara (PS) ya Ujenzi, marehemu Mariam El-Maawy.

Katika ujumbe wake wa faraja ambao nakala yake ilitumwa kwa vyombo vya habari, Rais Kenyatta alimtaja Mama Shariffa kama mzalendo aliyeitumikia taifa hili kwa miaka mingi na kwa kujitolea.

“Kama taifa tunamshukuru Mama Sharrifa kwa mchango wake katika maendeleo ya nchi haswa katika nyanja za elimu na afya.

“Mama Sharrifa ni miongoni mwa kundi la kwanza la wakunga waliosajiliwa nchini na ametoa huduma zake kwa miaka mingi kote nchini, haswa katika kaunti za Lamu, Garissa, na Kwale ambako pia alifunza wahudumu wengi wa afya,” akasema Rais Kenyatta.

Kiongozi wa taifa alisema Mama Shariffa alikumbatia elimu wakati ambapo ni wanawake wachache zaidi nchini walipata nafasi ya kunawiri kimasomo.

“Mama Sharifaa alikuwa ni kielelezo chema na mwanamke mkakamavu ambaye alifaulu kupata elimu ya kisasa wakati ambapo ni wanawake wachache waliweza kupata elimu ya kisasa,” Rais Kenyatta akaomboleza.

Kiongozi wa taifa aliomba Mungu aipe familia ya mwendazake nguvu ya kustahimili machungu ya kumpoteza.

Mariam El-Maawy alifariki mnamo Septemba 28, 2017 kutokana na majeraha aliyopata baada ya kushambuliwa na wafuasi wa kundi la kigaidi la Al shabaab katika mji wa Mpeketoni, kaunti ya Lamu.

Shambulio hilo lilitokea katika eneo la Milihoi katika ya Koreni na Hindi, umbali wa kilomita 40 kutoka mji wa Mpeketoni.

Gari lake lilisimamishwa kabla ya kushambuliwa kwa gurunedi ambapo aliokolewa na maafisa wa jeshi la Kenya (KDF) na Polisi.

  • Tags

You can share this post!

DINI: Dunia hii ina mitihani mingi, usitamauke, mtafute...

Waislamu walalamikia gharama ya juu ya maisha mwezi mtukufu...