• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 10:55 AM
Waislamu walalamikia gharama ya juu ya maisha mwezi mtukufu wa Ramadhani ukiwadia

Waislamu walalamikia gharama ya juu ya maisha mwezi mtukufu wa Ramadhani ukiwadia

Na KALUME KAZUNGU

WAUMINI wa dini ya Kiislamu, Kaunti ya Lamu wamelalamikia hali ngumu ya kiuchumi, ikiwemo ongezeko la bei za vyakula wakati huu ambapo mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani unaanza juma hili.

Waumini hao wanasema licha ya serikali kutangaza awali kwamba imeondoa ushuru unaotozwa kwa tende, walisema hatua hiyo bado haitoshi kwani vyakula vingi, ikiwemo mchele bado vinauzwa bei ghali.

Wakiongozwa na Ustadh Said Seif, waliiomba serikali kupitia Rais Uhuru Kenyatta kuangazia suala la bei za vyakula nchini na kuhakikisha zimepunguzwa.

“Tunashukuru kwamba sassa bei ya tende ni nzuri msimu huu wa Ramadhani lakini hiyo haitoshi. Vyakula vingi muhimu vinavyotumika wakati wa Ramadhani bado viko bei ghali. Ombi letu ni kwamba serikali isikie kilio chetu na kusukuma bei za vyakula kushukishwa,” akasema Bw Seif.

Naye Bw Is’haq Khatib alisisitizia haja ya serikali na wahisani kujitokeza na kusaidia familia zisizojiweza msimu huu wa Ramadhani.

Bw Khatib alisema janga la Korona limeathiri familia nyingi, ikizingatiwa kuwa wakazi wengi wamepoteza ajira kutokana na janga hilo.

“Waliokuwa tegemeo kwa familia wamepoteza kazi na hawawezi kukimu mahitaji ya familia. Tunapoingia mwezi wa Ramadhani, ningeomba serikali na wahisani kuzingatia kuzipa familia zisizojiweza msaada wa chakula ili pia zifurahie Ramadhani,” akasema Bw Khatib.

Waumini hao wa dini ya kiislamu pia waliisukuma serikali kulegeza kamba katika utekelezaji wa sheria zinazodhibiti makali ya Covid-19 nchini kipindi chote cha Ramadhani.

Ustadh Mohamed Abdulkadir aliomba serikali kubadili majira ya kafyu kutoka saa nne usiku hadi saa kumi alfajiri.

Ustadh Mohamed Abdulkadir. Picha/ Kalume Kazungu

Badala yake, Bw Abdulkadir alipendekeza saa hizo kusukumwa hadi saa tano za usiku ili kuwapa Waislamu muda wa kutosha kutekeleza sala mbalimbali msimu wa Ramadhani.

“Badala ya kafyu kuanza saa nne usiku, tunapendekeza ianze saa tano usiku hadi saa kumi alfajiri. Tunaamini wakifanya hivyo tutapata muda mwingi wa kutekeleza sala zetu,” akasema Bw Abdulkadir.

You can share this post!

Rais aomboleza kifo cha mamake aliyekuwa Katibu wa Wizara...

Kanisa Katoliki laitaka Kenya kusitisha mpango wake wa...