• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Kanisa Katoliki laitaka Kenya kusitisha mpango wake wa kufunga kambi za wakimbizi

Kanisa Katoliki laitaka Kenya kusitisha mpango wake wa kufunga kambi za wakimbizi

Na CHARLES WASONGA

SIKU chache baada ya mahakama kusimamisha, kwa muda, Kanisa Katoliki nchini limeshauri serikali ya Kenya kutofunga kambi za wakimbizi za Dadaab na Kakuma zinazohifadhi zaidi ya wakimbizi 500,000.

Kwenye taarifa, Muungano wa Maaskofu wa Kanisa hilo (KCCB) umesema ni muhimu kwa serikali kuendelea kuwapa hifadhi wakimbizi hao kwa sababu hawatakuwa salama katika mataifa asilia. Wengi wa wakimbizi hao wanatoka mataifa ya Somalia na Sudan Kusini.

“Hawa ni watu ambao maisha yao yamevurugwa kwa namna mbalimbali, ikiwemo usimamizi mbaya wa rasilimali, ukosefu wa asasi za utawala na siasa isiyokomaa. Isitoshe, wakimbizi hawa hawatakuwa salama katika nchi zao ambazo wakati huu zinakumbwa na mapigano na aina nyingine za uhalifu,” ikasema taarifa iliyoandikwa mnamo Aprili 9, 2021, na kutiwa sahihi na mwenyekiti wa KCCB Askofu Mkuu Philip Anyolo.

Maaskofu hao wametoa wito kuwe na mazungumzo kuhusu suala hilo kati ya serikali, Shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu Wakimbizi (UNHCR) na wadau wengine husika “ili kupatikane mwelekeo kuhusu suala hili.”

Muungano huo vile vile, umeitaka serikali kuimarisha usalama na usaidizi kwa wakimbizi hao huku wakitaka jamii ya kimataifa iisaidie Kenya kubeba mzigo wa kuwahudumia katika kambi zao.

Wito wa maaskofu hao unajiri baada ya Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i mnamo Machi 23 kuitaka UNHCR iandaa utaratibu wa kufunga kambi hizo. Alisema uwepo wa wakimbizi hao katika kambi za Dadaab na Kakuma umechangia ungezeko la visa vya utovu wa usalama katika maeneo ya karibu “na taifa la Kenya kwa ujumla”.

“Uwepo wa wakimbizi hawa pia umechangia uharibifu wa mazingira katika maeneo karibu na kambi hizo,” akasema Dkt Matiang’i

Kwa upande wake shirika hilo la wakimbizi lilikubali kuwahamisha wakimbizi hao katika mataifa ya Amerika, Canada, Sudan Kusini na Ethiopia. Kenya imeitisha mkutano mwingine na UNHCR wiki ijayo kujadili suala hilo kwa kina.

Jumla ya wakimbizi 512,494 wako nchini. Wakimbizi 224,462 wanaishi katika kambi ya Dadaab, 206,458 katika kambi za Kakuma na Kalobeyei na 81,574 ambao wanaishi katika maeneo ya miji.

You can share this post!

Waislamu walalamikia gharama ya juu ya maisha mwezi mtukufu...

ANC yadai ODM inamtisha Uhuru kwa kutisha kuungana na Dkt...