• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 3:25 PM
ANC yadai ODM inamtisha Uhuru kwa kutisha kuungana na Dkt Ruto

ANC yadai ODM inamtisha Uhuru kwa kutisha kuungana na Dkt Ruto

Na CHARLES WASONGA

MIPANGO ya ODM kubuni muungano na Naibu Rais William Ruto kuelekea uchaguzi mkuu wa 2022 ni njama ya chama hicho kumlazimisha Rais Uhuru Kenyatta kuunga mkono azma ya Raila Odinga ya kuwania urais, chama cha ANC sasa kinadai.

Kwenye taarifa kwa vyombo vya habari Jumapili, mwenyekiti wa chama hicho Kelvin Lunani alisema mazungumzo ambayo Gavana wa Kakamega Wycliffe Oparanya alikuwa nayo na Dkt Ruto katika mbuga ya Maasai Mara ni sehemu ya mpango wa kufanikisha ajenda hiyo.

“Pia hatua ya chama hicho kuonyesha undumakuwili kuhusu iwapo kingali kinaunga mkono handisheki au la ni sehemu ya njama. Hii inaonyesha kuwa ODM haikuwa na imani na mchakato wa BBI endapo haiendelezi masilahi yao finyu,” akaeleza Bw Lunani.

ODM imekuwa ikionyesha dalili za kwamba itafanya kazi na Dkt Ruto katika kila viongozi wake wanasema ni kulipiza kisasi kwa kile wanachodai ni “usaliti kutoka kwa Rais Kenyatta.”

Machi 2021 Seneta wa Siaya James Orengo, Mbunge wa Suna Mashariki Junet Mohamed na mwenzake wa Rarieda Otiende Amollo walidai kuwa Katibu katika Afisi ya Rais Karanja Kibicho anapanga kutenga Bw Odinga katika mipango ya urithi wa Rais Kenyatta kwa kuhujumu mchakato wa BBI.

Kulingana na Bw Lunani, ODM inajaribu “kubuni maadui kutoka nje” kama hatua kuokoa meli yake inayozama huku ikitoa taarifa za kukanganya iwapo Bw Odinga atawania urais au la.

“Njama hii ya kuwakanganya wafuasi wao na Wakenya kwa ujumla kuhusu mgombeaji wa urais wa ODM inaonyesha kuwa hakuna demokrasia ndani ya chama hicho. Vile vile, hali hii inaonyesha kuwa umaarufu wa ODM unadidimia kwa kasi mno,” akaeleza.

Wiki jana, mkurugenzi wa uchaguzi katika ODM Junet Mohamed alisema kuna mipango ya chama hicho kuandaa Mkutano wa Baraza Kuu la Kitaifa (NEC) ili itoa usemi wa mwisho kuhusu suala hilo ambalo limeendelea kuwakanganya wafuasi wake.

Mnamo Aprili 1, 2021, siku ya mwisho ambayo wanaotaka kugombea urais kwa tiketi ya chama hicho walipaswa kuwasilisha maombi yao, Bodi ya Kitaifa ya Uchaguzi (NEC) ilisema kuwa Bw Odinga, Oparanya na Gavana wa Mombasa Ali Hassan Joho ndio walikuwa wamewasilisha maombi yao.

Lakini siku moja baadaye Katibu Mkuu Edwin Sifuna alitoa kauli tofauti akisema Bw Odinga hakuwa amewasilisha maombi yake.

“Imekuwa msimamo wa Bw Odinga kwamba atazungumzia suala la uchaguzi mkuu wa 2022 baada ya kukamilishwa kwa mchakato wa BBI. Tangazo ambalo lilitolewa jana (Aprili 1, 2021) ilikuwa ni mzaha kwa ajili ya kuadhimisha Siku ya Wajinga (April 1 Fool’s Day),” akasema.

  • Tags

You can share this post!

Kanisa Katoliki laitaka Kenya kusitisha mpango wake wa...

Kiptanui na Tanui waibuka washindi wa Xiamen Siena Marathon