• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 2:16 PM
Fahamu muda sahihi unaopaswa kula matunda

Fahamu muda sahihi unaopaswa kula matunda

Na MARGARET MAINA

[email protected]

WATU wengi hula matunda wakati wowote wanapojisikia wao bila ya kutambua kuwa inatupasa kula matunda kipindi maalumu na pia hilo tunda inabidi liwe na sifa maalumu, sio kula tunda tu mradi ni tunda.

Watu wengi hupenda kula tunda kwa muda wanaoutaka wao au wanayala kwa kujikuta tu wanayala matunda pasipo kupanga au wengi wamejenga mazoea kula matunda baada ya mlo.

Kwanza inabidi tuzitambue faida za matunda katika miili yetu. Matunda yana faida nyingi sana kwa afya ya binadamu, hivyo yatupasa kuyapa kipaumbele mkubwa katika milo yetu ya kila siku.

Matunda ni chanzo kikubwa cha vitamini mwilini, hulinda mwili kwa kuongeza kingamwili, hupunguza uzani wa mwili kwa watu wanene, hulainisha ngozi, huondoa sumu mwilini, hufanya mishipa ya damu kusafirisha damu vizuri, huongeza na kuimarisha nguvu ya mwili na kadhalika.

Kula tunda kipindi ukiwa na njaa

Ukila tunda wakati tumbo liko wazi au unahisi njaa, husagika kwa urahisi. Baada ya saa moja au zaidi unaweza kula sasa mlo wako mwingine wa kawaida.

Usile matunda baada ya mlo

Watu wengi wamezoea kula matunda baada ya mlo kamili.Inaelezwa kuwa ulaji wa matunda baada ya mlo sio sahihi kwa sababu matunda huyeyuka haraka kuliko chakula cha kawaida . Tunda linapokuwa tayari kutoka tumboni kuelekea kwenye utumbo mwembamba huzuiliwa na chakula. Baada ya muda tunda huchanganyikana na chakula na kuoza na hatimaye huzalisha asidi ambayo humfanya mtu kuumwa tumbo baada ya kula matunda, lakini pia virutubisho vyake hupotea.

Ili kuepukana na hali hiyo ya msongamano kwenye tumbo, kula matunda saa moja kabla ya mlo au angalau masaa mawili baada ya mlo. ukizingatia utaratibu huo utakuwa umetoa nafasi ya chakula kusagika na bila kuzuia uyeyukaji wa matunda

Zingatia kiwango cha sukari kwa baadhi ya matunda

Baadhi ya matunda kama vile papai na ndizi mbivu yana kiasi kingi cha sukari. Ingawa karibu kila tunda huwa na sukari lakini baadhi yana kiasi kingi zaidi. Hivyo inashauriwa kula matunda kwa kiwango cha wastani kila siku .Aidha unapokula tunda hakikisha unakula kwa ukamilifu wake ili kupata virutubisho vyake. Kwa mfano unapokula chungwa hakikisha unakula pamoja na nyama zake ili kupata virutubisho vyote muhimu vilivyomo. Pia ulapo tango jitahidi baada ya kuliosha ule pamoja na maganda yake.

Jiwekee tabia ya kula matunda ya aina mbalimbali kwa nyakati tofauti ili kupata Vitamini na Madini tofauti tofauti kulingana na mahitaji ya mwili. Hii ni kwa kuwa matunda ndiyo yanayojenga na kuimarisha kinga ya mwili dhidi ya maradhi na kamwe hutasumbuliwa na magonjwa mara kwa mara.

You can share this post!

Raila Odinga, Rais Kenyatta watoa mamilioni kusaidia...

Ufugaji wa kuku riziki tosha kwake