• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 2:07 PM
MARY WANGARI: Udangayifu katika mitihani ni tishio kwa jamii nzima

MARY WANGARI: Udangayifu katika mitihani ni tishio kwa jamii nzima

NA MARY WANGARI

MITIHANI ya kitaifa imekuwa ikiendelea nchini huku ikiandamwa na sarakasi za kila aina ikiwemo madai ya udanganyifu.

Wakenya wameshuhudia visanga tele kuhusu mitihani ya KCPE na KCSE ambapo Waziri wa Elimu Profesa George Magoha ameripotiwa akisisitiza kuwa hakuna uvujaji wowote wa mitihani hiyo.

KCPE ilikumbwa na sakata ikidaiwa kuwa maswali katika mtihani wa Kiingereza yalidondolewa kutoka jaribio moja lililokuwa limechapishwa mnamo Februari, mwezi mmoja tu kabla ya mtihani huo kuanza.

KCSE haikunusurika huku baadhi ya wazazi na walezi wakiripotiwa kuwalipa watu wawafanyie watoto wao mitihani kikiwepo kisa cha mwalimu aliyechapisha karatasi ya mtihani kwenye mtandao wa kijamii wa WhatsApp.

Ni jambo la kuvunja moyo sana kuona sekta ya elimu nchini ikielekea kuzama licha ya mageuzi yaliyoanzishwa na Dkt Fred Matiang’i. alipokuwa waziri wa elimu.Enzi hizo, wazazi wangefanya chochote hata kama ni kinyume na sheria, ilmradi tu kuhakikisha watoto wao wanapita mitihani na kujiunga na taasisi za kifahari.

Si ajabu baada ya mageuzi hayo, matokeo katika shule nyingi tajika yalianza kudorora ghafla na kuzigeuza dhihaka, huku shule ambazo hata hazikuwa zikisikika zikianza kutia fora.

Kwa kiasi fulani, inaeleweka ni kwa nini wazazi na walezi hujitahidi kwa hali na mali kuhakikisha watoto wao wamenyakua nafasi katika shule nyota za sekondari zinazowahakikishia nafasi ya kujiunga na vyuo vikuu na hatimaye kupata kazi.

Hata hivyo, kutokana na udanganyifu katika mitihani, wanafunzi wengi werevu hasa kutoka mashinani hufungiwa nje na kukosa fursa ya kujiunga na vyuo huku nafasi zao zikitwaliwa na wasiozistahili.

Matokeo yake ni kuwa na wafanyakazi wasiofaa katika taaluma muhimu kama vile udaktari, uhandisi, ualimu, watumishi wa umma, wanasiasa na waundaji sera, huku sekta ya utafiti na uvumbuzi nchini ikiathiriwa pakubwa.

Udanganyifu katika mitihani hauathiri sekta ya elimu pekee bali jamii kwa jumla.Inahuzunisha kuwa jamii haithamini tena uadilifu na badala yake imegeukia kutukuza ukora ambao matokeo yake ni dhahiri kupitia kuongezeka kwa mafarakano ya kimahusiano, kifamilia ikiwemo ndoa kuvunjika.

Aidha, baadhi ya maafisa wanajinyakulia nyadhifa kuu kwa kutumia vyeti vya kughushi!Tunahitaji mfumo wa mitihani unaoangazia talanta, ujuzi na ari ya kila mtahiniwa kibinafsi ili kuboresha sekta ya elimu nchini na kuondoa ushindani usiokuwa na maana.

[email protected]

You can share this post!

Vigogo wapimana akili

Hofu msitu kugeuka uwanja wa mauti