• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 8:50 AM
Knec kuanza kusahihisha KCSE wiki hii

Knec kuanza kusahihisha KCSE wiki hii

Na VICTOR RABALLA

SHUGHULI ya kusahihisha Mtihani wa Kidato cha Nne (KCSE) wa mwaka huu itaanza wiki hii huku serikali ikianzisha mpango wa kusawazisha kalenda ya masomo.

Katibu wa Wizara ya Elimu Dkt Julius Jwan alisema, wasahihishaji watawasili Nairobi kuanzia mwishoni mwa Ijumaa kujiandaa kwa zoezi hili huku karatasi ya mwisho ya mtihani huo ikitarajiwa kufanywa Alhamisi wiki ijayo.

Dkt Jwan alisema hayo alipoongoza shughuli ya kufunguliwa kwa konteina na usambazaji wa karatasi za mtihani katika kaunti ndogo ya Bondo jana.

Alielezea matumaini kuwa Wizara ya Elimu itakomboa muda wa masomo uliopotea wakati wa janga la Covid-19. “Kuhusu mitihani iliyofanywa mapema, tunawatarajia wasimamizi wa usahihishaji na manaibu wao kusafiri hadi Nairobi kuanzia Ijumaa wiki hii ili waanze kujiandaa kwa shughuli hiyo muhimu,” akasema.

Dkt Jwan alisema baada ya maandalizi hayo, wasahihishaji wengine watakaoshiriki katika zoezi hilo watasafiri hadi Nairobi.Kulingana na ratiba ya mtihani wa KCSE 2020 iliyofanyiwa marekebisho, karatasi za mwisho za mtihani zitafanywa mnamo Aprili 21.

Karatasi hizo ni pamoja na Sayansi Kimu (Home Science), Sanaa na Maumbo, “Power Mechanics”, “Umeme”, Uchoraji, Teknolojia ya Usafiri wa Angani na Mafunzo ya Kompyuta.

Dkt Jwan vile vile, aliwaonya walimu, wazazi na watahiniwa dhidi ya kupotoshwa na walaghai wanaosambaza karatasi feki za mitihani ya KCSE katika mitandao ya kijamii.

Alisema wale waliokamatwa wiki jana ni miongoni mwa watu hao ambao wamekuwa wakiitisha pesa kutoka kwa watu wasiong’amua ukweli kuhusu uhalali wa karatasi hiyo.

Mmoja wa waliokamatwa ni mwanamke mmoja mkazi wa kaunti ya Machakos.

“Kufikia wakati watahiniwa walikuwa wakifanya mtihani wa Hisabati, karatasi ya Pili, wiki jana, karatasi ghusi zilikuwa zikisambazwa. Kwa bahati mbaya baadhi ya wenzetu walinaswa katika mtego huo na wakatuma pesa kwa walaghai hao,” Dkt Jwan akasema.

Katibu huyo wa Wizara alitoa hakikisho kuwa Wizara ya Elimu imeziba mianya yote ya kufanikisha wizi wa mtihani huo.

You can share this post!

Hofu msitu kugeuka uwanja wa mauti

CECIL ODONGO: Muungano wa Raila, Ruto utamtakasa Naibu wa...