• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 3:53 PM
CHOCHEO: Jifunze kuomba msamaha ili furaha irejee kwenye ndoa

CHOCHEO: Jifunze kuomba msamaha ili furaha irejee kwenye ndoa

NA BENSON MATHEKA

Wengi husema kuwa wanaume hawaombi wake zao msamaha wakiwakosea hata wakipatikana peupe wakichepuka lakini sivyo kwa Dan. Inasemekana kuwa wanawake ni wepesi wa kuomba msamaha wakikosea waume wao lakini sivyo kwa Elena. Wawili hawa ni mtu na mkewe na ndoa yao imekuwa yenye patashika nyingi kwa sababu ya tofauti zao.

Tofauti na wanaume wengine, Dan hupenda kuomba mkewe msamaha kila wakati akihisi amemkosea. Hafanyi hivi kwa sababu hawezi kukaa ngumu kama wanaume wengine wenye roho za chuma, ni kwa sababu anampenda mkewe na anatambua mchango wake katika maisha yake. Lakini kwa Elena mambo ni tofauti.

Anachukulia tabia ya mumewe ya kumuomba msamaha kama unyonge.“Mwanamume ngani huyu anayependa kusema “nisamehe” kila wakati. Nimemchoka. Siwezi kuomba msamaha hata akinipata peupe nikichepuka,” asema Elena ambaye amekuwa katika ndoa kwa miaka sita. Kwa George na Cindy, ndoa yao ya miaka 11 imedumu kwa sababu ya kuombana msamaha.

“Tunatambua kwamba binadamu ana mapungufu mengi na kwamba bila msamaha na kunyenyekea kwa mwenzako ndoa haiwezi kudumu. Hii haimaanishi mtu achepuke kwa sababu anafahamu akiomba mwenzake msamaha atamsamehe,” asema Cindy.

Katika maisha ya mapenzi, aeleza, kila kitu hakiwezi kuwa mteremko na inafika wakati vitendo, matamshi na hatua anazochukua mtu zikawa maudhi kwa mwenzake.

“Katika hali hii, kuomba msamaha ndio njia ya pekee ya kurejesha furaha katika ndoa. Hakuna haja ya kununiana kwa sababu ya kukosa kutamka maneno mawili au matatu “naomba msamaha mpenzi” na kutuliza hali,” asema George ambaye pamoja na mkewe ni washauri wa wanandoa katika kituo cha Abundant Life Care jijini Nairobi.

Kulingana na mtaalamu huyu, kuwa na roho ya chuma kunaweza kusababishia mtu mateso makubwa katika maisha ya mapenzi.“Najua mwanadada ambaye ametalikiwa mara tatu kwa sababu ya kuwa na roho ngumu hivi kwamba hawezi kuomba msamaha na kunyenyekea kwa mwanamume.

Najua mwingine ambaye ana cheo kikubwa tu na pesa lakini amekosa mume wa kumuoa kwa kuwa wanaume huwa wanamhepa kwa kuwa hawezi kunyenyekea kwao,” asema George. Wataalamu wa masuala ya mapenzi wanasema kwamba dawa ya kukuza mapenzi katika ndoa, ni kuombana msamaha kila wakati mtu akihisi kwamba amemkosea au kumuudhi mwingine.

“Hii ni tiba. Mwanamume, omba msamaha nawe mwanamke usichukulie ombi la mumeo la msamaha kama unyonge. Kwa hakika, mwanamume anayeomba mkewe msamaha ndiye dume kamili na anafaa kuheshimiwa kwa sababu sio wengi wanaofanya hivyo,” asema Joseph Kimani, mtaalamu wa kituo cha Maisha Mema jijini Nairobi.

Sheila Wanjiru, mwanadada mwenye umri wa miaka 25 asema alishtuka mumewe wa miaka mitano alipomuomba msamaha baada ya kumuudhi.

“Sikuamini, nilimkumbatia kwa furaha na kumbusu kwa kuwa ilikuwa mara ya kwanza katika maisha yangu kusikia mwanamume akiomba mwanamke msamaha, na sio mwanamke mwingine, mimi binafsi,” asema Wanjiru. Kulingana na mwanadada huyu, alichukulia hatua ya mumewe kama nguvu na akazidisha mapenzi

.“Tuko sawa, sijawahi kuona mume wangu akiwa na unyonge kwa sababu ya kuniomba msamaha. Ni dume na ninamheshimu sana kwa hilo,” asema. Ingawa Cindy anasema kwamba wanandoa wanafaa kuombana msamaha, anaonya wachumba kuwakosea wenzao makusudi kwa sababu wanafahamu watawasamehe wakiwaomba msamaha.

“Kosa la makusudi linaweza kuzua balaa. Haufai kutumia upole wa mtu wako kumnyanyasa zaidi kwa kurudia kosa ili akusamehe,” asema Cindy. Michael Ndegwa, mkazi wa mtaa wa Loresho, Nairobi asema kwamba alichoka na tabia ya mkewe ya kuhanya na kisha kuomba msamaha akifika nyumbani akiwa amechelewa.

“Ilifika mahali nikakataa msamaha wake. Alikuwa akinitumia vibaya na nikamtaliki,” asema. George asema mtu hafai kusamehe mchumba aliye na tabia zinazoweza kumtumbukiza kwenye hatari. “Kwa mfano, mtu hawezi kuwa anakupiga kila mara kisha akuombe msamaha ilhali amekuumiza,” asema.

You can share this post!

Mfumo mbadala wasaidia KRA kukusanya Sh21 bilioni

WANDERI KAMAU: Uamuzi kuhusu Sankara ulete mwanga mpya...