• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 5:07 PM
Tangatanga walia kuteswa na wandani wa Uhuru

Tangatanga walia kuteswa na wandani wa Uhuru

Na MWANGI MUIRURI

VIONGOZI wanaoegemea upande wa Naibu Rais William Ruto katika eneo la Mlima Kenya, wamedai kuhangaishwa wanapojiandaa kwa chaguzi ndogo zinazopangiwa kufanyika mwezi ujao eneo hilo.

Seneta wa Kaunti ya Murang’a, Dkt Irungu Kang’ata, amedai kuwa wanasiasa wanaomuunga mkono Rais Uhuru Kenyatta wamezindua njama zisizofaa kuvuruga nafasi ya Tangatanga kutwaa nyadhifa za maeneo-bunge ya Juja na Kiambaa pamoja na Wadi ya Muguga katika chaguzi ndogo zijazo.

Alidai kuwa, nia iliyopo ni kuhakikisha Dkt Ruto na wenzake hawatamwaibisha Rais katika ngome yake ya Kaunti ya Kiambu.

“Tulipewa kidokezo kuwa baada ya Mbunge wa Juja, Bw Francis Munyua kuaga na kisha diwani wa Muguga, Bw Eliud Ngugi akamfuata, kuliandaliwa mkutano wa dharura katika mkahawa mmoja ulio katika barabara ya kutoka Ruiru Kimbo hadi Nembu na ambapo iliazimiwa kuwa chaguzi hizo ndogo kwa vyovyote vile zisitawaliwe na Tangatanga,” akadai.

Kulingana naye, mambo hayo ndiyo yaliyomfanya Dkt Ruto kujitenga na chaguzi hizo ili asionekane kama anayetaka kukabiliana na Rais Kenyatta moja kwa moja ngomeni kwake.Aliwataka wapinzani wao wazingatie haki za demokrasia na kuwapa wananchi nafasi ya kujiamulia mkondo wanaotaka kufuata kisiasa bila shinikizo za vitisho na kuhangaishwa.

Hata hivyo, wafuasi wa Rais Kenyatta katika eneo hilo wamekuwa wakipuuzilia mbali lalama za wapinzani wao wakitaka wafuate sheria ikiwa hawataki kukamatwa na kushtakiwa kwa makosa waliyowahi kuyafanya.

You can share this post!

Nia yetu ni kuisaidia Kenya kumudu madeni – IMF

Hatimaye Uhuru atangaza nafasi za makamishna IEBC